KISA CHA MISHI, MAPENZI SI HESABU

KISA CHA MISHI, MAPENZI SI 
HESABU.     
                  
1.
Kwa jina naitwa Mishi, binti mwenye heshima,   
Mwenzenu ni mtumishi, nipo ofisi ya umma,
Kama hiyo haitoshi, mwanamke najituma,
Penzi halina kanuni, chunga usije kosea.
2.
Nina gari namiliki, mwenyewe sina dereva,
Ninayo nyumba Masaki, nina shamba Usariva,
Kwa fedha sibabaiki, nakula vilivyo iva,
Penzi halina kanuni, chunga usije kosea.
3.
Nina elimu si haba, UDSM nimesoma,
Shukurani zake baba, pongezi kwa wangu mama,
Kazi sasa yanibeba, umri nao wayoyoma,
Penzi halina kanuni, chunga usije kosea.
4.
Nimetafuta jamali, mwenzenu nataka mume,
Hata awe suruali, aso kitu kwa kuume,
Kikubwa awe rijali, simtaki gumegume,
Penzi halina kanuni, chunga usije kosea.
5.
Kila nilipo pakaa, matatizo hunipata
Tarasimu hazikufaa, kunikinga na matata,
Nikaja kata tamaa, huyo mtu sikumpata,
Penzi halina kanuni, chunga usije kosea.
6.
Penzi kiumbe habithi, mja naomba sikia,
Ninatendwa uhanithi, moyoni ninaumia,
Usije dhani hadithi, tena si tamthilia,
Penzi halina kanuni, chunga usije kosea.
7.
Sijui nianze mwisho, pale tulipogombana,
Na vile vyake vitisho, yaani vya kuachana,
Si lolote ni michosho, si ya leo si ya jana,
Penzi halina kanuni, chunga usije kosea.
8.
Vema nianzie mwanzo, pale tulipokutana,
Niwasimulie chanzo, mimi naye kushikana,
Mimi nilikuwa ponzo, alipogongwa kijana,
Penzi halina kanuni, chunga usije kosea.
9.
Ndipo ikanilazimu, mwili wake kuutibu,
Na ule umaamumu, ukamtoka taratibu,
Nikawa ninajihimu, kutazama matibabu,
Penzi halina kanuni, chunga usije kosea.
10.
Mgonjwa kawa mpenzi, bila hata kumaizi,
Akaanza kunienzi, taratibu kwa mapozi,
Nami nikawa mpanzi, sikuifanya ajizi,
Penzi halina kanuni, chunga usije kosea.
11.
Sijui nikawa wapi, sikuona mbalamwezi,
Nuru ilitoka vipi, na jua halichomozi,
Sijui dunia ipi, mapenzi kumbe uchizi,
Penzi halina kanuni, chunga usije kosea.
12.
Huyu Jamali muhibu, alikuwa yu chuoni,
Anasoma uhasibu, palepale Mlimani,
Bumu likileta tabu, humpiga kampani,
Penzi halina kanuni, chunga usije kosea.
13.
Sijiu ndio kudeka, au kuchuna jamani,
Mishi kile nakitaka, sina fedha mfukoni,
Ili nipate ridhika, nipatie wangu hani,
Penzi halina kanuni, chunga usije kosea.
14.
Nikakope kama sina, muhibu wangu apate,
Mwanafunzi kazi hana, niliwaza siku zote,
Kumbe mapenzi hakuna, kiumbe chuma ulete,
Penzi halina kanuni, chunga usije kosea.
15.
Pendo lake silipati, ubavuni hanitoki,
Pendo lake ni la chati, na kumuacha sitaki,
Nampenda kwa dhati, ila kwake sipendeki,
Penzi halina kanuni, chunga usije kosea..
16.
Kosa hakika si kosa, mbona atasema sana,
Ya zamani na ya sasa, wallahi yatajazana,
Mapenzi yananitesa, utulivu hata sina,
Penzi halina kanuni, chunga usije kosea.
17.
Huo wivu alonao, kama anipenda sana,
Situmii mitandao, uhuru mwenzenu sina,
Anipangia vikao, niende au hapana,
Penzi halina kanuni, chunga usije kosea.
18.
Kila siku twazozana, kama mafurusi sina,
Na leo tumegombana, sababu ni ndogo sana,
Akatalii uchina, nauli yenyewe hana,
Penzi halina kanuni, chunga usije kosea.
19.
Sina karma ya Mwasiti, mahaba ningeyavua,
Kama yangekua kiti, kalio ningeinua,
Nimezama katikati, mapenzi yaniumbua,
Penzi halina kanuni, chunga usije kosea.
20.
Kumuacha natamani, moyo wangu hautaki,
Hanipendi si utani, ila kwangu haondoki,
Anaruka kama Nyani, ubavuni habanduki,
Penzi halina kanuni, chunga usije kosea.
21.
Sijui niendelee, au hapa niishie,
Sasa twaenda uzee, yako mengi niwambie,
Naomba mtuombee, ndoa yetu itulie,
Shida ukizizoea, njia utajipatia.

Dotto Chamchua Rangimoto(Njano5)
Mzalendo.njano5@gmail.com
784845394/764845394
Morogoro Tanzania