MSUKUMA HABARI YAKO.


















MSUKUMA HABARI YAKO.
1
Mpemba sabalheri, unaionaje hali,
Kwangu mie ni buheri, namshukuru Jalali,
Usiwe na munkari, lijibu langu suali,
Kwanini wapenda shari, kama vile hauswali?
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
2
Mgogo habari yako, salamu zangu pokea,
Hapa nina swali lako, lile ulilo zoea,
Kuomba silika yako? jibu ninalingojea,
Lini unarudi kwako? Dom ulipotokea?
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
3
Mtumbatu nampenda, wenzangu naweka wazi,
Mtu huyu hana inda, tena hana utalazi,
Mwaminifu kama kunda, akiwa na laazizi,
Sishangae akikonda, sababu ya mkumbazi.
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
4
Mmakunduchi mpole, si mwepesi kuchukia,
Tena hapendi kelele, na fujo kuzisikia,
Aenda huku na kule, kuti ajitafutia,
Ila mvivu kwa shule, umande aukimbia,
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
5
Mzaramo sikupati, zinduka silale doro,
Uwate tupu kibeti, isifike yako soro,
Wapenda kichenipati, watoto wakosa karo,
Unalitunza kabati, nguo waweka kwa poro,
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
6
Msukuma simsemi, ila ukweli nampa,
Sio kwamba hajitumi, tatizo ni zake pupa,
Pombe ageuza maji, huku nguo azitupa,
Akifika kwenye lami, anayavua malapa.
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
7
Mnyakyusa kwa vioja, hakuna wa kumpata,
Fulusi anazifuja, kama vile aokota,
Aagizia mapaja, jikoni yalo tokota,
Anywa supu kwa mrija,soda kwake tarumbeta,
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
8
Mhaya apenda sifa, tena kupita kiasi,
Aweza lalia fafa, kibanda chake cha nyasi,
Pia asiwe na sofa, masikini si mkwasi,
Atatamba sio lofa, ana kasri Parisi
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
9
Mhehe si mchokoze, hasa yule wa Kalenga,
Tena simgombeze, usimfanyie ngenga,
Hujui na nikujuze, mwepesi wa kujinyonga,
Kosa lake mueleze, maneno ukiyachunga.
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
10
Mkuriya ana nini, leo nataka ukweli,
Kila siku gazetini, mara lile mara hili,
Kumwaga damu mwilini, kwake yeye ni sahali,
Ana tatizo rasini, kiasi aitwe nduli,
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
11
Mluguru kwa kulima, mwenzenu nampongeza,
Gimbimaji na mlima, kuchemsha anaweza,
Wali wake kama sima, wallahi hutaongeza,
Atasema kwa heshima, mkono umeteleza,
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
12
Mchaga toka Machame, aongoza ubahili,
Yu tayari akuchome, kikubwa apate dili,
Asemwa ni gumegume, ati ni yake asili,
Kama mate umteme, kiumbe huyu katili,
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
13
Mha atege sikio, nisemalo asikie,
Anajua kwenda mbio, lengo lake litimie,
Afanye watu fagio, njia wamsafishie
Apate mafanikio, awaacha wajifie.
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
14
Mkwere ana maneno, huyasema rejareja,
Kwa mithali na mifano, huzichanganya lahaja,
Kesha maliza matano, weye huna hata moja,
Vile bila ndoano, ajipatia kangaja,
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
15
Mnyamwezi kwa ushamba, nadhani atia fora,
Avae apige pamba, utacheka kama jura,
Akiwa alima shamba, anaruka kama chura,
BASATA wakimbamba, 'taungana na Snura.
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
16
Mdigo yule wa Tanga, asifika kwa kupika,
Uchungu wote wa chunga, kirahisi inalika,
Kwa mapenzi ndio nanga, ukizama hutatoka,
Ukikutoka ujinga, nguo anaziloweka,
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
17
Mpare wa milimani, analima tangawizi,
Anashangaza jamani, chai yake ya mluzi,
Haipiki na majani, yaani hata mizizi,
Wanayo fikira gani, mjue sijamaizi,
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
18
Mfipa kwake Mpanda, Mpimbwe na Sumbawanga,
Kibeku anakipanda, anapaa akiwanga,
Hufanya analopenda, kwa tunguri na usinga,
Akitaka kukuwinda, anakuchinjia ninga.
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
19
Mmakonde mla panya, ati samaki mchanga,
Leo mimi nakukanya, ndugu yangu wa Nambunga,
Hebu jaribu kufanya, uvue japo mkunga,
Rohoni nimekusinya, natamani kukutenga.
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
20.
Kaditama samahani, nyie nilio wakwaza,
Mimi ni wenu mtani, sio yule wa Vigwaza,
Natokea undambani, Ifakara si Muheza,
Msiweke mtimani, lengo si kuwachokoza.
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.

Dotto Rangimoto Chamchua(Njano5)
whatspp/call 0622845394 Morogoro.