KIRUSI CHA ZIKKA CHATINGA RASMI AFRIKA.


Serikali ya Guinea-Bissau imebuni kamati ya dharura ya afya baada ya kuripotiwa kesi tatu za kwanza za kirusi hatari cha Zika.

Taarifa ya Wizara ya Afrika ya nchi hiyo imesema kuwa, kesi za ugonjwa huo hatari zimeripotiwa katika eneo la Bijagos na kwamba serikali imebuni kamati maalumu inayoongozwa na Waziri Mkuu Baciro Dja ili kuzuia kusambaa kwa kirusi hicho, wakati huu ambapo nchi hiyo ndogo ya magharibi mwa Afrika inajikusanya baada ya kukumbwa na ugonjwa wa Ebola.

Kirusi hatari cha Zika kiliripotiwa kuibuka barani Afrika kwa mara ya kwanza katika Visiwa vya Cape Verde magharibi mwa bara hilo mwezi uliopita. Mkrugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) barani Afrika, Matshidisho Moeti alisema, kesi hiyo ya Cape Verde ni ushahidi kuwa kirusi cha Zika sasa kimesambaa hadi nje ya bara la Amerika na kuingia Afrika.

Kirusi cha Zika kuligunduliwa kwa mara ya kwanza barani Afrika mwaka 1947 na hakikuhesabiwa kuwa hatari hadi kilipoibuka upya mwaka jana nchini Brazil na kusababisha wanawake walioambukizwa kuzaa watoto wenye ubongo mdogo.

RWANDA YAIPINGA MAREKANI KUIHUSISHA MAGENDO YA BINADAMU.


Serikali ya Rwanda imekadhibisha tuhuma za Marekani kuwa inahusika na magendo ya binaadamu.

Mathilde Mukantabana, balozi wa Rwanda nchini Marekani hapo jana aliitaja ripoti hiyo kuwa ya kisiasa ambayo iko kinyume na ukweli wa mambo katika jamii ya Wanyarwanda wenyewe. Bi, Mukantabana ameogeza kuwa, serikali ya Kigali ina uwezo kamili wa kuwalinda na kuwapa hifadhi wakimbizi hususan raia wa Burundi.

Balozi huyo amefafanua kuwa, kuwalinda raia wa Burundi mkabala na kufanya magendo ya binaadamu, ni suala linalopewa kipaumbele na serikali ya Rwanda. Katika ripoti yake ya mwaka 2015 iliyotolewa siku ya Alkhamisi, Juni 30 Marekani iliituhumu serikali ya Kigali kwamba inashiriki katika magendo ya binaadamu hususan raia wa Burundi.

Kadhalika ripoti hiyo iliashiria kwamba Rwanda imekuwa ikiwatumia watoto wadogo wa Kirundi kama askari. Hii si mara ya kwanza kwa serikali ya Rais Paul Kagame kutuhumiwa kuhusika na vitendo vya ukandamizaji wa haki za binaadamu.

80 WAFA KWA MASHAMBULIZI YA MABOMU IRAQ.


Watu wasiopungua 80 wameuawa na wengine wengi kujeruhiwa katika mashambulizi pacha ya mabomu katika mji mkuu wa Iraq, Baghdad.

Hujuma ya kwanza imeripotiwa kufanyika alfajiri ya leo nje ya mgahawa mmoja katika wilaya ya Karada na muda mfupi baadaye shambulizi la pili likafuatia mashariki mwa Baghdad.

Kamati ya Usalama ya Mkoa wa Baghdad awali ilisema watu zaidi ya 60 wameuawa na wengine 100 wamejeruhiwa. Kundi la kigaidi la IS limekiri kuhusika na mashambulizi hayo na kutoa takwimu tofauti na za serikali za wahanga wa hujuma hizo. IS wamesema watu 40 wameuawa katika mashambulizi hayo na wengine 80 wamejeruhiwa.

Mashambulizi hayo yamefanyika masaa machache baada ya Waziri Mkuu wa Iraq kuzionya pande zinazowaunga mkono IS. Haider al-Abadi aliyasema hayo jana Jumamosi katika kikao na waandishi wa habari mjini Baghdad, na kuongeza kuwa, wale walioanzisha kundi la kigaidi la IS au kuliunga mkono, hivi sasa wanateketea katika moto ambao waliuwasha wao wenyewe.

Hujuma hii inafanyika siku mbili baada ya watu 46 kuuawa na kujeruhiwa katika shambulizi la kigaidi dhidi ya msikiti mmoja katika kitongoji cha Abu Ghraib, viungani mwa Baghdad, mji mkuu wa Iraq.

ASSAD: MGOGORO SYRIA UTAISHA KWA MAZUNGUMZO SAMBAMBA NA KUPAMBANA NA UGAID.


Rais Bashar Assad wa Syria amesema kuwa, haiwezekani kupatikana njia ya ufumbuzi halisi wa mgogoro wa nchi hiyo bila ya kuwepo mapambano ya kweli dhidi ya ugaidi.

Rais Assad amesema kuwa, kuna ishara za kukomeshwa mgogoro wa Syria na kuongeza kuwa, utatuzi wa mgogoro wa nchi hiyo unafungamana na mazungumzo ya Wasyria kuhusu mchakato wa kisiasa lakini sambamba na hayo mapambano dhidi ya ugaidi yanapaswa kudumishwa.

Kuhusu mwendo wa kinyonga wa mchakato wa kutafuta suluhisho la mogoro wa Syria, Rais Bashar Assad amesema: Waungaji mkono wa magaidi wa Magharibi na nchi kama Saudi Arabia, Uturuki na Qatar hazitaki kusitisha misaada yao kwa makundi hayo ya kigaidi. Rais wa Syria amesema iwapo misaada hiyo itasitishwa na Wasyria wakashauriana kuhusu katiba, mustakbali wa nchi na mfumo wa utawala basi hapana shaka kutapatikana utatuzi wa mgogoro huo hivi karibuni.

Baada ya kupita miaka 5 sasa tangu nchi ya Syria itumbukizwe katika mgogoro wa ndani, na kudumishwa misaada ya pande zote ya nchi za Magharibi na vibaraka wao kwa wapinzani na makundi ya kigaidi kwa shabaha ya kuiondoa madarakani serikali halali ya Rais Assad, sasa kumeanza kujitokeza ishara za kukomeshwa mgogoro huo.

Tangu mgogoro huo ulipoanza Marekani, Uturuki, Saudi Arabia na Qatar zilifanya kila liwezekanalo kuiondoa madarakani serikali halali ya Syria na kuwasaidia wanachama wa makundi ya kigaidi kuingia nchini humo. Ushirikiano wa miaka 5 wa nchi hizo na makundi ya kigaidi haujaweza kutimiza sehemu ndogo ya malengo yaliyoainishwa kwa ajili ya mgogoro wa Syria na hadi sasa Rais Bashar Assad angali anaongoza nchi hiyo huku makundi ya kigaidi yakidhoofika siku baada ya siku.

Inaonekana kuwa moja kati ya matunda ya uwekezaji wa nchi kama Uturuki katika mgogoro wa Syria ni kuhatarisha usalama wa Uturuki yenyewe ambayo miji yake mingi imekuwa ikikukmbwa na mashambulizi ya mara kwa mara ya milipuko ya kigaidi. Shambulizi la hivi karibuni kabisa ni lile la Jumanne iliyopita lililolenga uwanja wa ndege wa Ataturk mjini Istanbul na kuua watu karibu 50. Watu wengine zaidi ya 200 wamejeruhiwa.

Matokeo kinyume na matarajio ya mradi wa nchi za Magharibi na vibaraka wao katika mgogoro wa Syria yamezilazimisha nchi hizo kuanza kuamiliana na serikali ya nchi hiyo kama alivyosisitiza rais Assad kwamba nchi za Magharibi zinawatuma maafisa wao hususan maafisa wa masuala ya usalama huko Damascus ili kushirikiana na kufanya mazungumzo ya siri na Syria.

Wakati huo huo Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki amewaambia waandishi habari katika mji wa Sochi nchini Russia kwamba nchi yake inataka kutatuliwa mgogoro wa Syria kwa njia za kisiasa. Mevlüt Çavuşoğlu amesema Uturuki ilikuwa na mitazamo tofauti kuhusu suala la kubakia madarakani Rais Bashar Assad huko Syria lakini sasa iko tayari kufanya mazungumzo kuhusu mitazamo mingine.

Hata hivyo na kama alivyosisitiza Rais Bashar Assad wa Syria, matamshi matupu ya kutaka kuwepo utatuzi wa kisiasa wa mgogoro wa Syria hayatoshi na hapana shaka kuwa, mapambano ya kweli dhidi ya makundi ya kigaidi nchini Syria ni miongoni mwa masharti muhimu ya utatuzi wa kisaisa wa mgogoro huo.

Mafanikio ya Syria katika vita dhidi ya ugaidi ikishirikiana na Iran na Russia, yameimarisha nafasi ya Rais Assad na hapana shaka kuwa, usalama na amani ya nchi jirani vitaimarishwa kwa kuyaangamiza kikamilifu makundi ya kigaidi nchini humo.

MOHAMMAD PAKPOUR: MAREKANI NA SAUDIA ZILITUMA MAGAIDI KUSHAMBULIA IRAN.

Kamanda mwandamizi wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu la Iran IRGC amesema wanachama wa magenge ya kigaidi waliokamatwa hivi karibuni hapa nchini wakipanga njama za kutekeleza mashambulizi ya bomu wamekiri kwamba walipokea ufadhili kutoka Saudi Arabia na Marekani.

Brigedia Jenerali Mohammad Pakpour, kamanda wa kikosi cha ardhini cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu la Iran amesema magaidi hao wamekiri kuwa walifadhiliwa na nchi mbili hizo ili kujenga ngome hapa nchini na haswa katika maeneo ya mipakani kwa shabaha ya kutekeleza hujuma za kigaidi katika kona mbali mbali ya nchi.

Brigedia Jenerali Mohammad Pakpour amesema Washington na Riyadh zimekuwa zikiyafadhili na kuyaunga mkono magenge ya kigaidi kwa lengo la kuyumbisha usalama wa nchi sambamba na kusambaratisha Mapinduzi ya Kiislamu, njama ambazo amesema hazitazaa matunda.

Amongeza kuwa, mmoja wa magaidi hao waliokamatwa wiki jana katika mji wa Khash mkoani Sistan-Baluchistan ameaga dunia kutokana na majeraha aliyoyapata wakati wa operesheni ya kusambaratisha ngome yao.

Waziri wa Usalama Iran Mahmoud Alavi siku chache zilizopita alisema magaidi wakufurishaji waliokamatwa hivi karibuni walipanga kutekeleza mashambulizi katika maeneo 50 kote Iran na haswa mji mkuu Tehran.

Amesema kuwa magaidi hao walikuwa wameshaainisha maeneo 50 ya kutega mabomu na kwamba tayari walikuwa na kilo 100 za mada za miripuko; huku vikosi vya usalama vikifanikiwa kuzuia tani mbili za mada hizo ambazo magaidi walipanga kuingiza nchini.

Mbali na kukamata magaidi 10 miongoni mwao, Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu la Iran IRGC liliangamiza magaidi watano wa kundi la kigaidi la PJAK kaskazini magharibi mwa nchi. Vikosi vya usalama na ulinzi nchini vimetibua mashambulizi kadhaa ya kigaidi katika muda wa siku chache zilizopita.

NIMETAFAKARI SANA.

Kumekucha ni salama, ahsante mungu wangu,
Japo dede nasimama, na tete hatua zangu,
Nina kuomba Karima, nifike safari yangu
Nimezama fikirani, nawaza mie nawaza.

Jana sikupe hasira, leo sipate karaha,
Tena sifanye harara, kesho upate furaha,
Kiumbe fanya subira, kama wazitaka raha.
Nimezama fikirani, nawaza mie nawaza.

Aliyeumba kinyonga, ndiye kaumba farasi,
Lumbwi siwezi jinyonga, kulilia kwenda kasi,
Karima ndiye hupanga, ndogo nyingi na kiasi,
Nimezama fikirani, nawaza mie nawaza.

Namtazama jongoo, kunako miguu yake,
Ilivyo kama pongoo, ajabu ni mwendo wake
Kamzidi kangaroo, lakini si mbio zake,
Nimezama fikirani, nawaza mie nawaza.

Sijaona uwaridi, lisilo kuwa na miba,
Ama jambo maridadi, baya liwate kubeba,
Jua kuna kujirudi, ndio ikawepo toba,
Nimezama fikirani, nawaza mie nawaza.

Mja usiwe bahili, pia usifanye ria,
Ila sianguke chali, asama kusaidia,
Moyo usizidi hali, Mola alokujalia,
Nimezama fikirani, nawaza mie nawaza.

Kaditama namaliza, hapa natia kikomo,
Shika nilo yawaza, huenda tapata somo,
Kuuliza unaweza, zingatia yaliyomo,
Nimezama fikirani, nawaza mie nawaza.

Dotto Rangimoto Chamchua(Njano5)
Whatspp/call 0622845394 Morogoro

MAPENZI, NDOA, ROHO, MAJINI NA BINADAMU.

Ndoa nyingi huvunjika, na wapenzi wengi huachana kabla hata hawajafunga ndoa. Kabla ya ndoa kuvunjika na wapenzi kuachana hutokea visa vingi vya usaliti, ukigeugeu na chuki.

Mapenzi nini? Mahala pake hasa ni wapi? Asili yake wapi?Wakati gani usaliti hutokea? Wakati gani mtu anakuwa kigeugeu? Nini hasa chanzo cha chuki kwa wapenzi?

Hakuna maana moja ya mapenzi, ila vyovyote iwavyo mapenzi ni ile hali ya kuvumilia na kukubali mapungufu, udhaifu na karaha za mtu yoyote au hali yeyote au kitu chochote.

Mapungufu, udhaifu na karaha zinapokuwa za kiwango kikubwa na bado ile hali ya uvumilivu na kukubali ikaendelea kuwepo,basi hapo ujue kuwa kiwango cha mapenzi kiko juu sana, na kinyume chake ni kweli. Ukiona mtu yuko na mapungufu na mbaya zaidi ni kero kwako lakini bado wampenda basi ujue kuwa uko na mapenzina huyo mtu.

Mapenzi mahala pake ni moyoni; ambapo si lile pande la nyama lenye vyumba na mishipa ya kutoa na kuingiza damu, bali ni ile roho ambayo ndio asili ya nguvu zote zinazopatikana ndani ya mwili wa mwanadamu. Mwili wa mwanadamu tunaweza kufananisha na kompyuta.

Kopyuta imeundwa na mifumo miwili yenye kutegemeana ambavyo ni hardware na software. Vile vitu tunavyoweza kuvishika na kuviona ndio hardware na vile ambavyo hatuwezi kuviona wala kuvishika ni software. Software ndio huilazimisha hardware nini ifanye, na hardaware hupokea command toka kwa software.

Kwa upande wa mwanadamu kuna roho na mwili. Roho ndio huamuru kitu cha kufanya na katu mwili hauwezi kuiamuru roho kitu cha kufanya. Roho ni kama OS[Operating System] kwa kompyuta.

Kwa mujibu wa mapokeo ya dini za kikristo na kiislamu, mwili wa mwanadamu umeumbwa kutokana udongo, kisha mungu akupulizia pumzi yake kwenye hilo dongo hata likawa mwanadamu mwenye uhai.

Kama nilivyosema awali kuwa roho ni kama OS, na ndani ya OS huweza kuongezwa programu mbalimbali kulingana na uhitaji wa mtumiaji wa kompyuta, pia kwa mwanadamu pia huwa kuna viprogramu vidogodogo vinavyopatikana ndani ya ROHO.

Viproglamu hivyo vidogo vidogo ni kama vile vya kucheka,kununa, kuchukia, kutamani, kupenda, nk, Kila ROHO si lazima iwe na viprogramu hivi vyote, bali zingine huwa na hizi na hukosa zile na zingine hupata zile na hukosa hizi.

Kikubwa cha kufahamu ni kuwa mwanadamu hawezi kucheka kama hana hicho kiprogramu cha kumuwezesha kucheka, kama vile huwezi kuchezesha video kwenye kompyuta yako kama hauna programu ya kukuwezesha kuchezesha video. Watu wengine hawajui kununa na wengine hawajui kucheka pia, hiyo ni kwasababu hakuna kitu hicho cha kununa au kucheka kwenye roho zao. Upendo na chuki ni moja kati ya viprogramu vilivyopo kwenye roho.

SOUL MATE? Class mate humaanisha ni mtu ambaye umesoma naye darasa moja, naam, mlikutana huko darasani. Nini maana ya SOUL MATE? Hivi roho hukutana? Kwa mujibu wa dini ya kiislamu M/Mungu alianza kuziumba roho za viumbe vyote kabla hata ya kuumbwa ulimwengu na ziliishi miaka mingi kabla hata hazijatiwa au kupuliziwa kwenye miili ya viumbe hivyo. Hivyo basi huenda hizo roho zilikutana huko kwa mara ya kwanza.

Katika filamu ya kihindi inayoitwa Dil To Pagal Hai mtunzi ametueleza kuwa roho zimeumbwa katika jozi, yaani mbili mbli huku zikiwa zimenatana. Wakati wa kutiwa kwenye miili ya viumbe zikatenganishwa, moja ikatiwa kwa mwanaume na nyingine ikatiwa kwa mwanamke. Hizi roho mbili lazima zikutane, na kukutana kwenyewe ni kwa watu waliobeba roho hizo kuoana, na ndoa iliyofungwa na watu wenye hizi roho mbili[soulmate] katu hawawezi kuachana.

Usaliti? Kigeugeu? Mara baada ya M/mungu kupulizia pumzi yake kwenye mwili wa mwanadamu, baadaye na hii mara baada ya kutokea uasi mbinguni zikaingia pumzi zingine ngeni kwenye miili ya wanadamu. Pumzi hizi ni majini, au mashetani au mapepo. Hizi pumzi hufanya kazi kama roho ndani ya mwili. Nilisema huko juu kuwa roho huamuru mwili cha kufanya, hivyo na haya majini pia huamuru mwili cha kufanya.

Mkumbuke Hawa na Adamu hawakuwahi kufikiria japo kuusogelea ule mti wa kati, lakini baada ya pumzi mpya kumuingia hawa, si kwamba waliusogolea tu, lakini pia wakala na lile tunda. Roho ya mtu iliumbwa kwa mfano wa Mungu, na kiasilika haiwezi kutenda dhambi au kuacha kumtii Mungu, ila roho ngeni zilizo muingia ndio humfanya atende dhambi, ndio maana twaambiwa kuna pepo la uzinifu, uongo, wizi, na kubwa zaidi roho zetu halaumiwi kwa kutenda dhambi bali zinalaumiwa kwa kushindwa vita na shetani.

Kwakuwa ndani ya mwili tayari kuna roho, na kwakuwa hizi roho ngeni[majini] nazo huamrisha mwili, hivyo basi huwa panatokea mashindano mengi ya kiroho ndani ya mwili wa mwanadamu. Vita???

Mwili siku zote hutii ile roho iliyoshinda haijalishi hiyo roho ni ngeni au ile aloumbiwa mwanadamu. Mfano mwanadamu waweza kutoka kuoga kisha ukajikuta uko katika mtihani wa kuchagua nguo ya kuvaa, wakati mwingine waweza kuvaa nguo kabisa kisha ukajikuta waivua na kuivaa nyingine, ila hali ya kuchagua nivae hii au ile ni matokeo ya mashindano ya kiroho ndani ya mwili, Vita?

Hata katika kuchagua mpenzi pia hutokea mashindano ya kiroho ndani ya mwili. Unapochagua mpenzi na kuamua kuishi naye jua kuwa kuna roho imekushinikiza kufanya hivyo na si vinginevyo. Kwakuwa watu wote tuko na roho ngeni nyingi kwenye miili yetu, kwakuwa hizi roho hutofautiana nguvu kulinganana nyakati, na kwakuwa roho yenye nguvu kwenye wakati fulani ndio hutawala kipindi hicho, hivyo basi kiwango cha “mapenzi” ya mwanadamu kwa mwenza wake hubadilika kadiri roho zinazotawala mwili wa mwanadamu huyo zinavyobadilika;hapa ndipo usaliti na kigeugeu vinapozaliwa.

Wakati wampenda mwajuma elewa kuna kiprogramu[roho] ndani ya mwili wako kimekufanya umpende huyo mwajuma, hiyo roho ikizidiwa nguvu hata ikaingia roho ya kumpenda Asha lazima utamuacha mwajuma na kuanza kumpenda Asha. Hizi roho ngeni ndio hupelekea “soulmate” wakati mwingine zisikutane. Kama ile roho ya inayompenda Asha ikiendelea kutawala kwa muda mrefu hata mauti, basi huyo mtu atendelea kumpenda Asha hadi kifo chake.

Cha kuzingatia, ile roho inayomfanya John ampende Asha haiwezi kufaulu hadi Asha awe na roho inayompenda John. Ikiwa roho hizi ni "SOULMATE" basi mapenzi ya Asha na John hudumu daima, kama hizi roho si "soulmate" na hivyo mapenzi yao ni matokeo ya roho ngeni[majini] zilizopendana, kwa hivyo mapenzi hayo yatachuja na kupotea kabisa mara baada ya roho hizo kutolewa kwenye utawala na roho zingine.

Roho ngeni namaanisha majini au mapepo. Kila mwanadamu ana majini wengi na kila jini kuna mambo anapenda na kuna mambo anachukia, na kila jina kuna siku yake, mwaka wake na hata muongo wake wa kutawala. Pia kila jini ana nguvu zake za kikawaida alizoumbwa nazo na kuna majini wengine wana nguvu za ziada(uchawi)

MWISHO:
katika yote hayo juu, naomba rejea kitendo cha Kefa kumkana Yesu mara tatu, rejea usaliti wa Yuda Iskariote kwa Yesu, rejea vita vya maswahaba baada kifo cha Mtume Muhammad(s.a.w), pia rejea maisha yako kila siku. Utabaini bila jelezi kuwa usaliti, kigeugeu, mapenzi, urafiki, nk vinatawaliwa na majini na roho, na kwasababu hiyo miili yetu haina hiyari hata kidogo.

Siku nyingine nitafafanua uhusiano kati ya majina yetu na mahusiano mapenzi na ndoa. Kwanini watu wengine huchezesha herufi za majina yao au hubadili majina kabisa kwa lengo la kuimarisha ndoa na mahusiano.

PENZI JINI HATARI.
1
Penzi ni jini hatari, wa kutesa na kuua,
Huzibeba zote shari, za kiangazi na mvua,
Nina kuomba Qahari, miye asije niua,
Mahaba yanizuzua, mtima wata ghururi.
2
Penzi mganga mzuri, huponya wanougua,
Hukusanya nyingi heri, za mwezi hata za jua,
Kwa idhini Ya Jabari, aponye changu kifua,
Mahaba yanizuzua, mtima wata ghururi.
3
Mapenzi istiimari, hakika nimetambua
Baridi naona hari, meli mwenzenu mashua,
Asali kwangu shubiri, ninajuta kuyajua,
Mahaba yanizuzua, mtima wata ghururi.
4
Mapenzi ni zingifuri, kwa mja anayejua,
Narauka Alfajiri, naswali naomba dua,
Yarabi penzi la siri, lisije kuniumbua,
Mahaba yanizuzua, mtima wata ghururi.
5
Penzi si kama johari, huwezi kulinunua,
Si mchanga wa bahari, bure ukalichukua,
Thamaniye si mahari, mkaja hata jazua.
Mahaba yanizuzua, mtima wata ghururi.
6
Penzi halina jabari, si chuma la kuinua,
Uwe bondia hodari, pia laweza sumbua,
Huba zataka sukari, moyo upate kutua,
Mahaba yanizuzua, mtima wata ghururi.
7
Mapenzi jua qadari, uwaze na kuwazua
Alo lipanga Ghafuri, hakuna wa kupangua,
Hivyo hatuna hiyari, hata kama twaamua
Mahaba yanizuzua, mtima wata ghururi.
8
Mapenzi si kibatari, ni mshumaa tambua,
Nyonda apate fahari, mwenyewe unaungua,
Yengekuwa samsuri, wallahi ningeyavua,
Mahaba yanizuzua, mtima wata ghururi.

Dotto Rangimoto Chamchua(Njano5)
Whatspp/call 0622845394

BINT WA DESMOND TUTU AVULIWA UKASISI KWA KUOA MWANAMKE MWENZAKE.

Binti wa Desmond Tutu, kiongozi mashuhuri wa Kikristo wa Afrika Kusini amevuliwa joho la Ukasisi baada ya kuoa mwanamke mwenzake.

Uongozi wa Kanisa la Anglikana nchini humo umesema, Mchungaji Mpho Tutu-van Furth, Padri wa kanisa hilo amepokonywa leseni ya kuendesha shughuli za kanisa hilo ikiwemo misa, ubatizaji, ndoa na maziko kwa kuwa kanuni za kanisa hilo haziruhusu ndoa za jinsia moja.

Binti huyo amesema babake Desmond Tutu, aliyekuwa Askofu Mkuu wa Kanisa la Angilkana nchini humo na pia mwanamapambano mashuhuri wa sera za kibaguzi hajashangazwa na habari hizo ingawa hazijafurahia.

Mpho Tutu alifunga ndoa na raia wa Uholanzi kwa jina Marceline, ambaye ni Profesa wa Tiba ya Watoto huko jijini Amsterdam Disemba mwaka jana, huku sherehe za harusi zikifanyika mjini Cape Town nchini Afrika Kusini mapema mwezi huu. Wanandoa hao waliwahi kuolewa huku nyuma na wote wana watoto.

Ni vyema kuashiria hapa kuwa, licha ya kuwa Kanisa la Angilikana linapinga liwati na usagaji, lakini Afrika Kusini iliidhinisha ndoa za jinsia moja mwaka 2006.

NDEGE YA MISRI ILIDUNGULIWA NA ISRAELI?

Uwezekano kuwa ndege ya abiria ya Misri iliyotoweka hivi karibuni ilitunguliwa na ndege za kivita za Israel, umezidi kupata nguvu.

Gazeti la al Misri al Yaum limeandika kuwa, uchunguzi unaonesha kwamba, kuna uwezekano mkubwa ndege ya abiria ya Egypt Air ilitunguliwa na ndege za kivita za utawala wa Kizayuni wa Israel.

Matamshi rasmi ya viongozi wa Ugiriki kuhusiana na ajali ya ndege ya abiria ya Misri na sababu zake, yamekwepa kwa makusudi kutaja mazoezi ya kijeshi ya utawala wa Kizayuni yaliyokuwa yanafanyika kusini mwa kisiwa cha Crete cha Ugiriki.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, mazoezi hayo ya kijeshi yalifanyika katika kalibu ya mpango wa mafunzo ya ndege za kivita za Israel kwa kutumia mipaka ya angani ya Ugiriki na katika mpaka wa Misri na Libya. Israel iliiomba pia Uturuki iruhusu kutumia anga yake, lakini Uturuki ilikataa.

Gazeti hilo la Misri limeongeza kuwa, ramani ya eneo la mazoezi hayo ya ndege za Israel inaonesha kuwa, ndege hiyo ya Misri ilipita katika eneo hilo wakati mazoezi yakiwa yanaendelea na ilitoweka katika rada dakika 27 baada ya kuanza mazoezi hayo ya kijeshi ya Israel.

KUVURUGA KWA SIMBA, MO ATOA YA MOYONI.


Michezo ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) imemalizika hapo jana na Simba SC ikijikuta ikiangukia nafasi ya tatu baada ya kupokea kichapo cha goli 2-1 kutoka kwa JKT Ruvu na hivyo kusalia na alama 62 huku Azam wakifikisha alama 64 na kushika nafasi ya pili baada ya kutoa sare ya goli 1-1 na Mgambo JKT,

Shabiki wa damu wa Simba, Mohammed Dewji ‘MO’ ameamua kufunguka yaliyo moyoni mwake kutokana na matokeo hayo.

Mara baada ya kumalizika kwa mchezo wa Simba na JKT Ruvu, MO ambaye pia ni Rais na Mkurugenzi Mtendaji wa Makampuni ya Mohammed Enterprises Tanzania Limited (METL Group) alitoa yaliyo moyoni kwake kuhusu Simba kupitia ukurasa wake wa Twitter, ujumbe ambao ulionekana kuwagusa mashabiki wa Simba na wadau wengine wa michezo nchini.

MO aliandika

“#Simba mnatunyima raha, tumechoka kutaniwa na kutukanwa mitaani”

BREAKING NEWS: KITWANGA ATUMBULIWA


Rais Magufuli ametengua uteuzi wa Waziri wa Mambo ya Ndani Mh. Charles Kitwanga kwa kosa la kuingia Bungeni akiwa amelewa

ALIYEANDIKA MWANYANGE APINDUE NCHI ATIWA MBARONI.

Jeshi la polisi mkoa wa Arusha linamshikilia mwanafunzi wa mwaka wa tatu wa Chuo cha Maendeleo ya Jamii Tengeru aliyejulikana kwa jina la Harold Mmbando (23) kwa kosa la kutoa taarifa za uchochezi dhidi ya Rais wa Zanzibar Dkt. Ali Mohamed Shein na Mkuu wa majeshi Jenerali Davis Mwamunyange.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha Charles Mkumbo alisema kuwa mtuhumiwa alitenda kosa hilo Mei 17 mwaka huu saa 09:00 asubuhi .
Ameeleza kuwa mtuhumiwa alaindika haya katika mtandao wa Facebook

“Mwamunyange pindua nchi haiwezekani wote wawe nje halafu hakuna aliyepewa mamlaka ya kukalia kile kiti.”

Aidha mtuhumiwa aliandika ujumbe mwingine kuwa

,”Dkt Shein akiuawa kama Karume sitashangaa wala kushtuka naomba Mungu mauaji ya kisiasa yaliyotokea Zanzibar yawe kwa viongozi wa kisasa hasa watawala na sio wananchi wa kawaida”.

Kamanda wa Polisi alisema kuwa, ni vyema wananchi wakatumia mitandao kwa njia iyakayolisaidia taifa badaala ya kutumia kusambaza jumbe za matusi au uchochezi kwani watajikutaka katika mazingira magumu.  

WEMA SEPETU: ALI KIBA WANGU MUMUACHE TU.

Wema Sepetu amezidi kuonyesha mapenzi aliyonayo kwenye kazi za msanii Alikiba na kusema huwa zinamkosha sana na kudai hajawahi kumuangusha siku zote

"Ila huyu bichwa wangu mimi ananikoshaga sana. Na mumuachage tu kwakweli. Bichwa una sifa lakini maana si kwa Vocal hizi. Halafu mimi siwezi kukubania namba bana. Naupenda sana huu wimbo jamani. Wajua kutukunaga mashabiki wako. Good work Bichwa wangu Officialalikiba did it again ladiez & Gentlemen"  aliandika Wema Sepetu

Mbali na hilo Wema Sepetu amempa pongezi msanii Alikiba kwa kuweza kusaini mkataba chini ya kampuni ya muziki ya 'Sony Music' na kusema kuwa alistahili hilo na zaidi ya hilo kwani anakipaji kikubwa.

" God Grants accordingly... Congrats Bichwa wangu for that Big Contract... You deserve it & more... Time Heals all wounds... The Sky remains to be the only Limit for u baba..." 

NDEGE YA MISRI YASEMEKANA ILIDUNGULIWA NA MAGAIDI.


Maafisa nchini Uigiriki wanasema vipande viwili “vinavyodhaniwa kuwa mabaki ya ndege ya iliotoweka ya Misri

"yameonekanayakielea katika bahari ya Mediterranean", bado haijabainika kama kweli ni ya ndege hiyo.

Waziri wa uchukuzi wa Misri r Sharif Fathi anasema kuna uwezekano mkubwa kwamba ndege hiyo “iliangushwa na magaidi”, lakini hakuna uwezekano mkubwa wa matatizo ya kiufundi.

Maafisa nchini Uigiriki wanasema ndege hiyo Airbus A320, iligeuka “ nyuzi 90 kushoto na kisha nyuzi 360 kulia kabla ya kutumbukia baharini kutoka umbali wa futi 27, 000.

Rais wa Ufaransa Francois Hollande amesema ndege hiyo nambari MS804, ilianguka.

HATIMAYE, NDEGE YA MISRI IMEANGUKA BAHARINI.

Hatimaye imethibitika ndege ya Misri imeanguka baharin,juhud za kusaka mabak zaendelea huku kukiwa na hisia za kigaidi.

Ndege hiyo aina ya Airbus A320 ya shirika la ndege la Misri la EgyptAir, iliyokuwa ikitoka mji mkuu wa Ufaransa Paris hadi Cairo awali iliripotiwa kutoweka kutoka kwenye mitambo ya rada.

Ndege hiyo ilikuwa imebeba abiria 66,na miongoni mwao kulikuwa na watoto 3,wafanyakazi watatu wa usalama na wahudumu saba.

Ndege hiyo ilipaa angani saa 11:09 usiku na ilitoweka ikiwa kilomita 16 ndani ya anga ya Misri na kupoteza mitambo ya rada saa 2:45 asubuhi,afisa mmoja katika shirika hilo la ndege alisema.

Sasa imethibitika ndega hiyo kuanguka bagarini na Operesheni ya kutafuta ndege hiyo imeanzishwa.

TAARIFA ZA SASA KUHUSU NDEGE YA MISRI ILOPOTEA.


Wanajeshi wa Misri na maafisa wa Uigiriki wanatafuta ndege ya shirika la EgyptAir iliotoweka ikitoka mjini Paris Ufaransa kuelekea Cairo Misri ikiwa na abiria 66.

Ugiriki imetuma ndege mbili na pia itatuma meli moja eneo hilo ili kusaidia utafutaji kwenye bahari ya Mediterranean ambako inaaminika huenda ndege hiyo ilianguka.

Nchini Ufaransa mamlaka zinaandaa mkutano wa dharura kujadili kutoweka kwa ndege hiyo.

Waliokuwemo kwenye ndege hiyo aina ya Airbus A320, ni pamoja na Wamisri 30 Wafaransa 15, Mwingereza 1, Mbelgiji 1,Wairaqi 2, Mkuwait 1, Msaudi 1, Msudan 1,Raia wa Chad 1,Mreno 1,Raia wa Algeria 1, na raia wa Canada 1.

Ilikuwa ikisafiri kutoka Ufaransa kwenda Misri na kutoweka kwenye mtambo wa rada kilomita 280 hivi kabla ya kufika pwani ya Misri.

Rais wa Ufaransa Francois Hollande na mwenzake wa Misri Abdul Fattah al-Sisi wamewasiliana na kuahidi kushirikiana katika uchunguzi, hayo ni kwa mujibu wa shirika la Reuters .

NDEGE YA MISRI YAPOTEA KWENYE RADA, HAUJULIKANI ILIPO

Ndege ya abiria ya shirika la EgyptAir iliyokuwa imebea abiria 56 na wahudumu 10 wakiwemo marubani imetoweka kwenye rada, ikitokea mji mkuu wa Ufaransa Paris kuelekea Cairo, mji mkuu wa Misri.

Gazeti la serikali la Ahram limeripoti kuwa, ndege hiyo yenye nambari ya usajili A320, ilikuwa inaruka umbali wa mita 11,300 kabla ya kutoweka kwenye rada, mashariki mwa bahari ya Mediterranean, maili 10 kabla ya kuingia kwenye anga ya Misri. Maafisa wa Idara ya Safari za Anga nchini Misri wamesema yumkini ndege hiyo imeanguka katika bahari hiyo.

Kwa mujibu wa Wizara ya Uchukuzi ya Misri, abiria waliokuwa kwenye ndege hiyo ni pamoja na Wamisri 30, raia 15 wa Ufaransa na Muingereza mmoja.

Itakumbukuwa kuwa, ndege nyingine ya abiria ya shirika la Metrojet la Russia nambari A321, ilianguka katika Peninsula ya Sinai nchini Misri Oktoba 31 mwaka jana, na kuua watu wote 224 waliokuwemo kwenye ndege hiyo.

Aidha ndege nyingine ya abiria ya shirika la EgyptAir iliyokuwa na abiria 55 na wahudumu 7 ambayo ilikuwa inatoka Alexandria kwenda jijini Cairo, ilitekwa nyara na raia wa Misri ambaye aliaminika kuwa na akili taahira kwa jina Seifuddin Mustafa ambaye alidai kuwa alifanya hivyo ili kuishinikiza serikali ya Cairo iwaachie huru wafungwa wa kisiasa kabla ya kubadili kauli yake na kusema kuwa alitaka aletewe mtalaka wake raia wa Cyprus waonane katika uwanja wa ndege wa kisiwa hicho.  

Mama mzazi wa binti aliyebakwa Morogoro alitumiwa video na kuipeleka polisi

Mama mzazi wa binti mmoja mkazi wa Dakawa wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro hivi karibuni alipokea ujumbe wa picha ya video katika simu yake ya mkononi na haraka aliifungua akiwa na shauku ya kuitazama.

Lahaula! Shauku yake ya kuitazama video hiyo aliyodhani ni sawa na nyingine za matukio ambazo amekuwa akiziona zikisambazwa mitandaoni, iligeuka huzuni na fedheha kubwa alipoona ikimwonyesha bintiye akidhalilishwa na wanaume huku akilalamika asirekodiwe bila mafanikio.

Mama huyo alijizoazoa haraka na simu yake akatimua mbio hadi Polisi kuripoti tukio hilo lililolenga kumdhalilisha binti yake na kuifedhehesha familia nzima. Hicho ndiyo kiini cha vijana 11 wa Dakawa kukamatwa ili waisaidie Polisi kuhusu walioshiriki tukio hilo na walioisambaza video hiyo kwa mama huyo na kwenye mitandao ya kijamii hasa WhatsApp.

Katika video hiyo, wakati mwanamme mmoja akimdhalilisha huyo binti, mwingine alikuwa akirekodi na baada ya kukamilisha tendo hilo lisilo na utu tena bila huruma waliwatumia watu wengine katika eneo la Dakawa.

Mkuu wa Wilaya ya Mvomero, Betty Mkwasa aliliambia gazeti hili jana kuwa miongoni mwa watu wa kwanza kuona video ile alikuwa mama wa msichana. “Alikimbia polisi kwenda kutoa taarifa,”alisema Betty.

Baada ya kufika Polisi, Betty alisema polisi walimwambia mama huyo hawawezi kuandika maelezo hadi mhusika ambaye ni binti yake afike kituoni. Walisema hivyo kwa sababu ni mtu mzima hivyo anatakiwa kutoa maelezo mwenyewe. Saa chache baada ya kuandikisha maelezo yake, polisi waliwakamata vijana wawili kwa tuhuma za kuhusika na unyama huo. Betty alisema watuhumiwa hao walikamatwa juzi na leo watafikishwa mahakamani.

Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Morogoro, Ulrich Matei alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba suala hilo linaendelea kufanyiwa kazi na kwamba hadi jana watuhumiwa 11 walikamatwa kuhusiana na tukio hilo.

Kamanda Matei alisema tisa kati yao wanaoshikiliwa ni kwa kosa la kusambaza picha za utupu huku vijana wawili ambao ni Zuberi Thabiti (30) na Iddy Adamu (32) ni kwa kosa la kufanya mapenzi na msichana huyo kwa nguvu huku wakirekodi.

Ilivyokuwa

Akisimulia tukio hilo, Kamanda Matei alisema kuwa watuhumiwa hao walifanya kitendo hicho Aprili 28 mwaka huu majira ya saa 1.00 usiku katika nyumba ya kulala wageni yenye jina la ‘Titii’ iliyopo Dakawa.

Kamanda Matei alisema kuwa binti huyo aliitwa kwenye nyumba hiyo ya wageni na Thabiti ambaye ni mkazi wa Mbarali wilaya ya Mbeya ambaye alikuwa na uhusiano naye kimapenzi. Baada ya kuingia chumbani alimkuta pia Adamu mkazi wa Makambako, Njombe ambao walimlazimisha kufanya mapenzi huku mmoja akimrekodi picha za video na baadaye kuzisambaza kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii.

Wanaoshikiliwa kwa kosa la kusambaza picha za utupu ni Rajabu Salehe (26), Said Athman (26), Musi Ngai (36), Said Muhammed (24), John Peter (24), Hassan Ramadhan (27), Ramadhan Ally (26), Lulu Peter (38) na Magreth Njonjone (30).

Wote ni wakazi wa Dakawa, Morogoro na wamevunja Sheria ya Makosa ya Mitandao, kifungu namba 14, kifungu kidogo (1) (a)

Kamanda Matei alisema wakati wa tukio hilo watuhumiwa hao walimtisha binti huyo kwa kisu ili asipige kelele wakati akidhalilishwa na walimtaka asitoe siri hiyo vinginevyo watamuua.

Kamanda alisema wawili hao ni marafiki wa msichana huyo na kwamba Thabiti ambaye ni mpenzi wa sasa wa msichana huyo alipanga na Adamu ambaye ni mpenzi wake wa zamani kumkomesha.

Alisema Thabiti alimwambia mpenzi wake wakutane hotelini. Msichana alipofika aliwakuta chumbani huku Adamu akiwa ameshika kisu na kamera. “Wakamlazimisha afanye vile na kumtishia kumuua kama angekataa,”alisema Matei.

Hata hivyo, Betty alisimulia kisa hicho na kusema watuhumiwa hao walifanya unyama huo kwa sababu ya usaliti wa mapenzi. Alisema msichana alidaiwa kujihusisha kimapenzi na dereva wa mpenzi wake.

Kwa mujibu wa Betty, baada ya mpenzi wake kugundua alipanga njama ili kuwakomoa wote wawili. Alisema mpenzi wake alimwambia wakutane hotelini na alipofika alimkuta Zuberi pamoja na dereva wa mchumba wake hotelini.

“Akawambia wafanye kile kitendo huku akirekodi video,”alisema Betty. “Nia yake ilikuwa kuwakomoa…kwa nini atembee na dereva wake,”alisema Betty na kwamba baada ya hapo picha hizo zilianza kusambaa.

Akizungumzia tukio hilo, Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk Hellen Kijo-Bisimba alisema hali hiyo inaonyesha jinsi maadili yanavyozidi kuporomoka katika jamii.

“Hilo siyo kosa la kisheria peke yake ni udhalilishaji mkubwa,”alisema.

Dk Hellen alisema licha ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu kukemea suala hilo ni vyema jamii ikazingatia suala la maadili.

Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA), Edda Sanga alisema vyama vya kutetea haki za wanawake vinafanya mkutano wa pamoja kujadili suala hilo.

“Leo (jana) tumekutana ili tujadili na kuja na tamko la pamoja,”alisema Sanga na kuongeza kwamba jambo hilo halivumiliki kwa sababu vitendo kama hivyo vinaendelea kujitokeza mara kwa mara.
  • Imenukuliwa kutoka gazeti MWANANCHI

RWANDA: HATUJA WATIMUA WAKIMBIZI.


Serikali ya Rwanda imekanusha madai kwamba, imewafukuza kutoka nchini humo wakimbizi kutoka Burundi.

Taarifa ya serikali ya Rwanda imesisitiza kwamba, haijawafukuza wakimbizi kutoka Burundi na kwamba wanaofukuzwa kutoka nchini humo ni raia wa Burundi wasio na vibali vya kuishi nchini humo.

Gavana wa jimbo la kusini mwa Rwanda ambako zaidi ya raia 1000 kutoka Burundi wamekwishatimuliwa ameziambia duru za habari kwamba, wanaofukuzwa walitakiwa kupata vibali vya kuendelea kuishi nchini humo na kisha warejee ikiwa watapenda.

Hivi karibuni Gavana wa mji wa Kirundo wa Burundi ambao uko katika mpaka wa nchi hiyo na Rwanda alisema kuwa, Rwanda imewatimia wakimbizi 1,300 wa Burundi ambao walitakiwa kurejea katika kambi za wakimbizi au kuondoka nchini humo. Melchior Nankwahomba alisema wale waliokataa kwenda katika kambi za wakimbizi walikuwa wakiondolewa kwa nguvu na maafisa wa Rwanda.

Makumi kwa maelfu ya Warundi walikimbilia Rwanda tangu ghasia zilipoanza nchini mwao mwaka mmoja uliopita, kufuatia uamuzi wa Rais Pierre Nkurunziza wa kuwania Urais kwa muhula wa tatu mfululizo hatua ambayo ililalamikiwa na wapinzani waliosema ilikiuka katiba na makubaliano ya amani ya Arusha Tanzania.

Burundi imekuwa ikiituhumu Rwanda kwamba, inaingilia masuala yake ya ndani, madai ambayo yanakanushwa na serikali ya Kigali.

KENYA YAPATA PIGO LINGINE, BAADA YA BOMBA LA MAFUTA, SASA RELI.


Rwanda imetangaza kuwa itajenga njia ya reli ya kisasa aina ya SGR kupitia Tanzania badala ya Kenya ikisema kuwa njia ya Tanzania itahitaji bajeti ya chini ikilinganishwa na Kenya.

Akihutubia waandishi wa habari hapo jana, waziri wa fedha wa Rwanda Claver Gatete, aliongeza kuwa itachukua muda kidogo kujenga reli hiyo kupitia Tanzania badala ya Kenya.

Utafiti uliofanywa na nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki umeonyesha kuwa njia ya Tanzania itagharimu Rwanda kati ya dola milioni 800-900 huku njia ya Kenya ikigharimu dola bilioni moja. Njia hiyo ya reli itakayotoka Dar es Salaam-Isaka-Kigali/Keza-Musongati (DIKKM) itakamilishwa mwaka wa 2018 na inatarajiwa kugharimu nchi husika jumla ya dola bilioni 5.2.

KISO CHAKO HUKISHIKI

Ufanye uende mbio, kaskazi mashariki,
Ubebe na kuku kwio, kwa ndumba unihiliki,
Yote yawa kifagio, kwa uwezo wa Maliki,
Jalali sio babio, elewa sihadhiriki.
Kiso chako hukishiki, hata kwa lake shikio.

Mja kalisha kalio, hazina pato shiriki,
Fanya uweke fungio, huta zuia riziki
Waja angua kilio, useme na hizo chuki,
Mola wangu kimbilio, wallahi sifedheheki,
Kiso chako hukishiki, hata kwa lake shikio.

Nimegundua mwenzio, tabasamu lako feki,
Watia kinukajio, kwa chips na mishikaki,
Umepaka kipambio, sumu nipate fariki,
Rabi kahuluku "sio" ndio mana sianguki
Kiso chako hukishiki, hata kwa lake shikio.

Ulo nalo kusudio, fahamu halisomeki,
Uweke na kikingio, kiso chako hukishiki,
Ingia kwa kitubio, umrudie Razaki,
Jalali kaumba "ndio" kwahivyo sitetereki.
Kiso chako hukishiki, hata kwa lake shikio.

Wanisema kwa wenzio, vile isivyo stahiki,
Mithili ya kisusio, mdomoni sikutoki,
Neno mwenziwe sikio, halichomi si mkuki,
Mungu tanipa tulio, hakika sibabaiki.
Kiso chako hukishiki, hata kwa lake shikio.

Umeshika mchinjio, na bado haushutuki,
Chakughuri kilalio, kiumbe hauzinduki,
Punguza matamanio, dunia haibebeki,
Rabi nipe kifutio, nifute zako falaki
Kiso chako hukishiki, hata kwa lake shikio.

Alokupa mtwangio, na kinu simdhihaki,
Kuna siku ya chungio, kiumbe huiepuki,
Hivyo situpe dekio, kesho haitabiriki,
Hapa pana zingatio, wajibu nduguye haki,
Kiso chako hukishiki, hata kwa lake shikio.

Dotto Rangimoto Chamchua(Njano5)
0622845394 Morogoro

ISRAELI YAFANYA MASHAMBULIZI UKANDA WA GAZA.


Wanajeshi wa utawala wa Kizayuni kwa kushirikiana walowezi wa Kizayuni wenye chuki za kidini na kitaifa, wamefanya mashambulizi katika maeneo tofauti ya Ukanda wa Ghaza na Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan dhidi ya Wapalestina.

Shirika la habari la WAFA limeripoti habari hiyo na kuongeza kuwa, wanajeshi wa utawala wa Kizayuni walioko katika mpaka unaotenganisha Ukanda wa Ghaza na ardhi nyingine za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu na Wazayuni, leo asubuhi wamevunja makubaliano ya kusimamisha vita kwa kuwashambulia wakulima wa Kipalestina, mashariki mwa Khan Yunus na kusini mwa eneo hilo, na kuwazuia kuingia kwenye mashamba yao.

Aidha leo asubuhi, wanajeshi wa utawala wa Kizayuni wamewashambulia kwa risasi wakulima wa Kipalestina mashariki mwa eneo la al Shujaiyya, katika Ukanda wa Ghaza.

Hadi sasa hakuna habari zozote zilizotangazwa kuhusu hasara iliyosababishwa na mashambulizi hayo ambayo ni uvunjaji wa wazi wa makubaliano ya kusimamisha vita.

Wakati huo huo walowezi wa Kizayuni leo wamezivamia nyumba za Wapalestina katika mji wa al Khalil wa kusini mwa Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan.

Licha ya walowezi hao wa Kizayuni kusaidiwa na wanajeshi wa utawala wa Kizayuni katika uvamizi huo, lakini Wapalestina wamesimama kidete kukabiliana nao, jambo ambalo limezusha mapigano baina ya pande hizo mbili.

WANANCHI WA YEMEN WASISITIZA KUPAMBANA NA MAREKANI.


Imam wa Sala ya Ijumaa iliyosaliwa jana huko San'a, mji mkuu wa Yemen amesema kuwa, wananchi wa nchi hiyo wataendelea kusimama kidete kupambana na wavamizi wa nchi yao.

Televisheni ya al Maseera ya Yemen imetangaza habari hiyo leo Jumamosi na kumnukuu Sheikh Abdul Majid al Houthi akiwaonya wanajeshi wa Marekani walioivamia ardhi ya Yemen kwamba wananchi wa nchi hiyo kamwe hawataruhusu hata shibri moja ya ardhi ya nchi yao ikaliwe na wavamizi.

Imam wa Sala ya Ijumaa ya San'a ameongeza kuwa, Marekani ina lengo la kuigawa vipande vipande nchi ya Yemen, lakini wananchi wa nchi hiyo wataendelea kuwa kitu kimoja mbele ya njema za Marekani.

Siku chache zilizopita, duru za habari za Yemen zilitangaza habari ya kuingia helikopta 15 aina ya Apache na helikopta 5 aina ya Black Hawk za jeshi la Marekani katika kambi ya jeshi la anga ya al Anad, kusini mwa Yemen.

Siku ya Jumamosi ya wiki iliyopita pia, wanajeshi 200 wa Marekani waliingia katika Ghuba ya Aden sambamba na kuwasili manowari ya kivita ya Marekani katika ghuba hiyo.

Imam wa Sala ya Ijumaa ya mjini San'a amesema, uvamizi huo wa Wamarekani nchini Yemen ulitabiriwa tangu zamani na wananchi wa nchi hiyo na ndio maana kwa zaidi ya mwaka mmoja sasa waendelea kukabiliana na wavamizi wa nchi yao.

BODABODA WANNE WAFA KWENYE MAANDAMANO HUKO CONGO DRC


Watu wanne wameripotiwa kuuawa katika maandamano ya waendesha pikipiki dhidi ya askari wa barabarani, huko mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Maandamano hayo yaliyoitishwa kwa ajili ya kulalamikia miamala mibaya ya polisi wa barabarani, yalifanyika katika barabara kuu ya eneo la Mambasa katika mkoa wa Orientale, kaskazini mashariki mwa nchi hiyo. Waandamanaji hao wanawatuhumu polisi kwamba wanachukua kiasi kikubwa cha fedha sawa na faranka 2000 kwa pikipiki moja ili kuruhusiwa kupita kwenye moja ya vizuizi kwenye eneo hilo, kiwango ambacho wanadai ni kikubwa kulingana na kipato chao.

Aidha madereva hao wa pikipiki (maarufu kama bodaboda) wametaka pia kuachiliwa huru pikipiki kadhaa ambazo zinashikiliwa na jeshi hilo la polisi wa barabarani katika eneo hilo. Katika kumaliza maandamano hayo, polisi hao wa barabarani walifyatua risasi kuwalenga waandamanji. Kiongozi wa eneo hilo la Mambasa, Alfred Bongwalanga amethibitisha kutokea machafuko hayo na watu wanne kuuawa.

Bongwalanga amesema kuwa, zaidi ya madereva 500 wa pikipiki walishiriki katika maandamano hayo. Baadhi ya vyombo vya habari vimesema kwamba, kulikuwa kumeshuhudiwa moto kwenye kituo kimoja cha polisi, kabla ya polisi kudhibiti eneo la PK51 katika mji huo wa Mambasa.

RWANDA YAKANUSHA KUHUSIKA NA MACHAFUKO YANAYO ENDELEA BURUNDI.

Serikali ya Rwanda imetoa ufafanuzi kuhusiana na tuhuma dhidi yake kwamba, imekuwa ikichochea machafuko katika nchi jirani ya burundi.

Rais Paul Kagame wa Rwanda amekanusha madai dhidi ya nchi yake kwamba, inawasaidia waasi wa Burundi kama ilivyokuja katika ripoti ya siri iliyowasilishwa kwa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.

Rais Kagame amesisitiza kuwa, nchi yake haiwasaidii kwa namna yoyote ile waasi wa Burundi au kuhusika na machafuko yanayoendelea kushuhudiwa katika nchi hiyo jirani. Rais Kagame amebainisha kwamba, machafuko ya ndani nchini Burundi chimbuko lake ni masuala ya ndani ya nchi hiyo.

Imeelezwa katika ripoti ya siri iliyowasilishwa kwa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kwamba, Rwanda imekuwa ikiwasaidia waasi wa Burundi wanaotaka kuiangusha serikali ya Rais Pierre Nkurunziza.

Ripoti hiyo ya wataalamu wa Umoja wa Mataifa inaeleza kwamba, Rwanda imekuwa ikiwasaidia kifedha, kimafunzo na hata kilojistiki waasi hao wanaopigana dhidi ya serikali ya Bujumbura.

Imeelezwa kuwa, Rwanda inafanya hivyo ili kuiondoa madarakani serikali ya Rais Nkurunziza.

Lambert Mende Omalanga ambaye ni msemaji wa serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo pia anaamini kuwa, serikali ya Rwanda imewapatia fedha waasi wa Rais Joseph Kabila ili kuwaimarisha.

Mende Omalanga amesema kuwa, Rwanda imekuwa ikiwapatia fedha wanachama wa kundi la zamani la waasi wa M23 ambao walisambaratishwa Novemba mwaka 2013 na kwa sasa baadhi yao wanaishi uhamishoni katika nchi za Rwanda na Uganda.

Ripoti ya siri ya wataalamu wa Umoja wa Mataifa iliyopelekwa katika Baraza la Usalama imefichua kwamba, waasi wa Burundi walioko mashariki mwa DRC wamekiri kwamba, katikati mwa mwaka jana walipatiwa mafunzo na watoaji mafunzo ambao baadhi yao walikuwa ni wanajeshi wa Rwanda.

Ripoti hiyo ya wataalamu wa Umoja wa Mataifa inakinzana na matamshi ya hivi karibuni ya viongozi wa Magharibi. Viongozi hao walidai kwamba, serikali ya Rwanda ilisimamisha himaya yake kwa waasi wa Burundi tangu mwaka jana.

Wataalamu wa Umoja wa Mataifa wanasema kuwa, wameipatia serikali ya Rwanda ushahidi unaoonesha juu ya kuweko ushirikiano wa siri kati yake na waasi wa Burundi na wa Congo DR. Aidha serikali ya Burundi ikishirikiana na jirani yake Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo imesema kuwa, ina nyaraka zinaoonesha juu ya kuweko harakati za siri za Shirika la Kiintelijensia la Rwanda. Pamoja na hayo serikali ya Rwanda imeendelea kukana kuhusika kwa namna yoyote ile na machafuko ya jirani yake Burundi.

Burundi ilitumbukia katika rangaito na mchafukoge Aprili mwaka 2015 baada ya Rais Pierre Nkurunziza kuidhinishwa na chama chake cha CNDD-FDD kuwania kiti cha Urais kwa mara ya tatu mfululizo.

Licha ya kuweko upinzani wa asasi za kiraia nchini Burundi na hata za kieneo na kimataifa, Nkurunziza alishiriki katika uchaguzi huo na kuibuka na ushindi na hivyo kushika hatamu za uongozi wa nchi hiyo kwa mara ya tatu mfululizo.

Kuendelea upinzani na maandamano kuliibua machafuko katika jiji la Bujumbura na miji mingine mikubwa ya nchi hiyo.

Takwimu zinaonesha kuwa, watu 500 wameuawa na wengine karibu laki mbili na 60 elfu wamekuwa wakimbizi tangu nchi hiyo ilipotumbukia katika machafuko hayo.

Katika kipindi chote hiki tangu Burundi itumbukie katika mgogoro wa kisiasa, wachambuzi wa masuala ya kisiasa wamekuwa wakitoa indhari mara chungu nzima juu ya hatari ya nchi hiyo kutumbukia katika vita vya ndani na vya mauaji ya kimbari.

Katika mazingira kama haya ya kutia wasiwasi, himaya ya kifedha na kijeshi kwa makundi yanayofanya fujo nchini Burundi au katika nchi jirani ni sawa na kumwagia mafuta ya petroli moto unaowaka.

AMNESTY YATAKA UGANDA IMKAMATE RAIS OMAR AL BASHIR.


Mashirika ya kimataifa ya kutetea haki za binadamu yameitaka serikali ya Uganda kumkamata Rais Omar al-Bashir wa Sudan na kumkabidhi kwa Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ICC, kwa tuhuma za mauaji ya kimbari katika eneo la Darfur na jinai dhidi ya binadamu.

Mashirika ya kutetea haki za binadamu ya Amnesty International na Human Rights Watch yameitaka serikali ya Uganda kutekeleza wajibu wake wa kimataifa na kumkabidhi kwa mahakama ya ICC, Rais wa Sudan ambaye alienda mjini Kampala kuhudhuria hafla ya kuapishwa Rais Yoweri Museveni.

Muthoni Wanyeki, Mkurugenzi wa Amnesty International katika kanda ya Afrika Mashariki, Pembe ya Afrika na eneo la Maziwa Makuu amesema Uganda ni mwanachama wa Mkataba wa Roma uliobuni Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ICC na hivyo, iwapo itafeli kumkabidhi Rais wa Sudan, itakuwa imeshindwa kutekeleza wajibu wake wa kimataifa. Hii ni katika hali ambayo, baada ya kula kiapo hapo jana, Rais Museveni aliikashifu ICC na kusema kuwa mahakama hiyo imegeuka na kuwa chombo cha kuwadhalilisha viongozi wa Kiafrika huku ikiwasaza viongozi makatili wa nchi za Magharibi. Kauli ya Museveni iliwaghadhabisha wajumbe wa Marekani na Umoja wa Ulaya waliokuwa wamehudhuria sherehe za kuapishwa kwake katika Viwanja vya Kololo jijini Kampala na kuwafanya kuondoka kwenye hafla hiyo.

Itakumbukwa kuwa, serikali ya Afrika Kusini ilikataa kumkamata Rais Omar al-Bashir ambaye alishiriki mkutano wa viongozi wa Afrika uliofanyika mjini Johannesburg Julai mwaka jana. Aidha Kenya ilipuuza wito wa kumkamata na kumkabidhi kiongozi huyo kwa Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai ICC anakotakiwa kujibu tuhuma za mauaji ya kimbari katika eneo la Darfur na jinai dhidi ya binadamu; alipohudhuria sherehe za kuapishwa Rais Uhuru Kenyatta wa nchi hiyo ya Afrika Mashariki mwaka 2013.

HIZBULLAH YACHUNGUZA KIFO CHA KAMANDA WAKE.


Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Lebanon ya Hizbullah imesema imeanzisha uchunguzi kubaini namna kamanda wake mwandamizi alivyouawa katika kile kilichotajwa kuwa hujuma ya jeshi la utawala wa Israel.

Taarifa ya Hizbullah imesema kuwa, harakati hiyo imeanzisha uchunguzi kubaini iwapo Mustafa Badruddin aliuawa katika hujuma ya anga ya jeshi la utawala wa Kizayuni wa Israel katika moja ya kambi za harakati hiyo karibu na uwanja wa ndege wa Damascus au la.

Taarifa hiyo imeongeza kuwa, uchunguzi wao unalenga kujua iwapo kamanda huyo mwandamizi aliuawa katika shambulizi la kombora au roketi, baada ya sauti kubwa ya kishindo kusikika jana katika kambi hiyo.

Ripoti za awali zilikua zimearifu kuwa Mustafa Badruddin, kamanda mwandamizi wa Hizbullah ya Lebanon aliuawa katika hujuma ya anga ya ndege ya utawala wa Israel.

Badruddin mwenye umri wa miaka 55 na ambaye alikua mkuu wa tawi la kijeshi la Harakati ya Kiislamu ya Lebanon Hizbullah, alikuwa akiongoza kikosi kinachoisaidia serikali ya Rais Bashar al-Assad wa Syria kupambana na makundi ya kigaidi katika nchi hiyo ya Kiarabu.

Kamanda huyo ambaye pia alikua mshauri wa Hassan Nasrullah, Katibu Mkuu wa Hizbullah na mkuu wa kitengo cha kiintelijensia, alikua binamu ya Imad Mughniyah, kamanda mwandamizi wa zamani wa Hizbullah ambaye aliuawa na kitengo cha ujasusi cha utawala wa Israe Mossad, mwaka 2008 katika mji mkuu wa Syria.

MAGAID WA DAESH WAUA WANAJESHI 17 WA IRAQ.


Takriban askari 17 wa jeshi la Iraq wameuawa katika shambulizi la bomu lililofanywa na kundi la kigaidi  la Daesh katika mkoa wa Anbar, magharibi mwa nchi hiyo.

Duru za kijeshi zinaarifu kuwa, magaidi hao jana Alkhamisi walilishambulia kwa mabomu gari la kijeshi katika wilaya ya Jarayshi, yapata kilomita 10 kutoka Ramadi, makao makuu ya mkoa wa Anbar na kuua askari 17 wa jeshi la serikali.

Imearifiwa kuwa, lengo la hujuma hiyo ya magaidi wa Daesh ni kukata mawasiliano kati ya eneo la Ramadi na Tharthar, lililoko kilomita 120 kaskazini magharibi mwa mji mkuu Baghdad ili kuwazuia wanajeshi wa Iraq kusonga mbele na kukomboa maeneo ambayo yanadhibitiwa na kundi hilo la kigaidi.

Aidha raia wawili waliuawa jana Alkhamisi katika hujuma tofauti ya kundi la kigaidi la Daesh katika eneo la al-Obeidi, mashariki mwa Baghdad.

Hujuma za jana zimefanyika siku moja baada ya magaidi hao kutekeleza shambulizi jingine lililosababisha makumi ya watu kupoteza maisha.

Siku ya Jumatano, watu wasiopungua 64 waliuawa na wengine zaidi ya 85 kujeruhiwa katika mripuko wa bomu uliotokea karibu na soko la Urayda katika kitongoji cha Sadr mashariki mwa mji mkuu wa Iraq, Baghdad.

RAIS WA GUINEA BISSAU AMFUTA KAZI WAZIRI MKUU.


Rais José Mário Vaz wa Guinea-Bissau amempiga kalamu Carlos Correia, Waziri Mkuu wa nchi hiyo na kutangaza kuivunja serikali.

Akilihutubia taifa jana Alkhamisi, Rais Vaz alisema serikali ya Correia imeshindwa kuupatia ufumbuzi mgogoro wa kisiasa uliopo na kubuni taasisi zinazoendana na matakwa ya utawala wake.

Rais José Mário Vaz wa Guinea-Bissau amevitaka vyama vya siasa kushauriana na kumteua Waziri Mkuu mpya.

Correia alipewa jukumu la kuwa Waziri Mkuu wa nchi hiyo ndogo ya magharibi mwa Afrika mwezi Oktoba mwaka jana, akiwa ni kiongozi wa tatu kushikilia wadhifa huo ndani ya muda wa miezi mitatu. Correia kama wenzake wawili waliomtangulia, alitazamiwa na utawala wa Rais Vaz kuupatia ufumbuzi mzozo wa kisiasa unaotokota nchini humo unaodaiwa kuripuka kuanzia ndani ya chama tawala cha PAIGC.

Mapema mwezi Machi mwaka huu, Ujumbe wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ulioitembelea nchi hiyo kwa ajili ya kuchunguza hali ya mambo, umeyasema hayo wakati wa mazungumzo na Rais wa Guinea-Bissau, José Mário Vaz, Spika wa Bunge na viongozi wa vyama vya kisiasa.

Mgogoro wa kisiasa nchini Guinea-Bissau umekuwa mkubwa kiasi cha kufanya upatanishi wa Jumuiya ya Uchumi ya Nchi za Magharibi mwa Afrika (ECOWAS) na Jumuiya ya Nchi Zinazozungumza Lugha ya Kireno (CPLP) kushindwa kumaliza mivutano hiyo ya kisiasa

KAMANDA WA HEZBOLLAH AMEUAWA.

Kundi la wapiganaji la Hezbollah limesema kuwa kamanda wake wa juu,Mustafa Badreddine ameuawa katika shambulio la anga la Israel nchini Syria,Vyombo vya habari vimeripoti.Mustafa Badreddine anadaiwa kuhusika na mauaji ya Waziri mkuu wa Israel Rafiq Hariri mwaka wa 2005.

VIRUS VYA EBOLA HUJIFICHA HUISHI KATIKA SHAHAWA.


Utafiti waonesha kuwa virusi vya Ebola vinaweza kuishi katika shahawa ya wagonjwa wanaopona kwa mwaka mzima

Taasisi ya Pasteur ya Ufaransa imetoa taarifa ikisema, utaifiti moja uliofanywa na watafiti wa Ufaransa na Guinea unaonesha kuwa virusi vya Ebola vinaweza kuishi katika shahawa (sperms) za wagonjwa wanaopona kwa mwaka mzima.

Utafiti huo unafanywa na taasisi ya Pasteur, Taasisi ya maendeleo ya Ufaransa, Taasisi ya afya na matibabu ya Ufaransa na mashirika ya utaifi ya Guinea. Matokeo ya utafiti huo yametolewa katika jarida la “Maradhi ya kuambukiza” la Marekani.
Watafiti waliwachunguza wagonjwa 450 wa Ebola waliopona kwa mwaka mazima, na kuchambua majimaji ya mwili wao, yakiwemo machozi, mate na shahawa.

Uchambuzi wa sampuli za shahawa 98 ya wagonjwa 68 waliopona unaonesha kuwa kufuatia ongezeko la uponaji wa wagonjwa hao, idadi ya virusi vya Ebola katika shahawa zao inapungua. Katika mwezi mmoja hadi mitatu baada ya kupona kwa wagonjwa, asilimia 28.5 ya shahawa ina virusi vya Ebola; Baada ya miezi 7 hadi 9, kiwango hicho kinapungua hadi asilimia 6.5; baada ya miezi 12, virusi vya Ebola vikatoweka katika shahawa.

Hivyo, watafiti wanapendekeza wagonjwa wa Ebola wanopona katika miezi kadhaa baada ya kupona wanatumia mpira wakati wa ngono, na kushauri masharika husika kufuatilia afya za wagonjwa hao, ili kuepuka maambukizi ya virusi hivyo kuibuka tena.

NEWCASTLE NA NORWICH ZIMESHUKA DARAJA.


Ushindi wa Sunderland wa 3-0 dhidi ya Everton Jumanne uliwafikisha hadi alama 38 na kwa kuwa Norwich na Newcastle hawawezi kuwafikia, moja kwa moja klabu hizo mbili zikashushwa daraja.

Kwa sasa Norwich wana alama 34 sawa na Newcastle. Klabu nyingine iliyoshushwa daraja ni Aston Villa iliyo na alama 17 kwa sasa.
Troy Deeney alikuwa amewapa Watford uongozi mechi hiyo iliyochezewa Carrow Road lakini Norwich wakajibu kupitia bao la Nathan Redmond.

Dieumerci Mbokani aliwafungia Norwich la pili naye Craig Cathcart akawaongezea la tatu kwa kujifunga.

Odion Ighalo alikomboa bao la pili lakini Mbokani akawafungia Norwich bao la nne.
Baada ya kushushwa daraja, Norwich sasa watakuwa wakichezea tu fahari mechi yao ya mwisho dhidi ya Everton Jumapili.

WA KIMATAIFA KUIFUATA ESPERANCA JUMAPILI.


Yanga itaondoka Dar es Salaam siku moja tu baada ya kukabidhiwa Kombe la ubingwa wa Ligi Kuu ya Soka Tanzania Bara katika mchezo dhidi ya Ndanda FC ya Mtwara Uwanja wa Taifa.

Bodi ya Ligi Kuu Tanzania Bara (TPLB) imeidhinisha mchezo Ndanda na Yanga kuchezwa Uwanja wa Taifa, badala ya Nangwanda Sijaona, Mtwara baada ya klabu hizo kukubaliana.

Yanga inatarajiwa kucheza na wapinzani wao, Sagrada Esperanca ya Angola kati ya Mei 17 au 18 mwaka huu Katika mchezo wa kwanza ulifanyika Dar es Salaam Jumamosi iliyopita ambapo Yanga iliwafunga wageni wake mabao 2-0 Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Yanga inahitaji ama sare, ushindi na kama kufungwa basi si zaidi ya bao moja ili kuindoa Esperanca katika hatua ya awali, ili kuingia hatua ya makundi katika kusonga mbele.

Wakati huo huo Rais wa Shirikisho la Soka nchini TFF Jamal Emil Malinzi ameipongeza Yanga kwa kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Soka Tanzania Bara kwa mara ya pili mfululizo baada ya kufanya hivyo msimu uliopita wa mwaka 2014/2015.

Hii ni mara ya 26 kwa Yanga kutwaa taji tangu kuanza kwa Ligi Kuu Tanzania Bara mwaka 1965, ikifuatiwa na Simba iiliyotwaa mara 18 na Mtibwa Sugar ya Morogoro mara mbili.

Yanga imefikia rekodi hiyo baada ya kutwaa ubingwa katika miaka ya 1968, 1969, 1970, 1971, 1972, 1974, 1981, 1983, 1985, 1987, 1989, 1991, 1992,1993, 1996, 1997, 1998, 2002, 2005, 2006 na misimu ya 2007-2008, 2008-2009, 2010-2011, 2012-2013, 2014-15 na 2015-16.

Kwa upande mwingine Malinzi pia amezikumbusha na kuhamamisha klabu zitakazoshiriki Ligi Kuu msimu wa 2016/17 kutoa maoni na mapendekezo, ili kuboresha kanuni za uendeshaji wa ligi hiyo kwa msimu ujao.

Yanga imetwaa ubingwa huo ikiwa na mechi mbili mkononi, dhidi ya Ndanda Jumamosi na Majimaji Mei 22 Uwanja wa Majimaji, Songea.

POPE: MASHABIKI WA SIMBA WAMEHARIBU TIMU.


Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya klabu ya Simba Zacharia Hanspope amewashutumu mashabiki kuwa ndio chanzo cha timu hiyo kufanya vibaya.

Hans pope amesema, kwa upande wa mechi za Simba na Yanga haziangalii ubora wa timu kwani zinamambo yake mengi sana na wao kama Simba walijiamini kuchukua ubingwa kutokana na mwenendo wa timu ulivyokuwa tangu mwanzo wa Ligi.

Pope amesema, kufanya vibaya kwa timu kumeanza katika mchezo wa Robo fainali ya Kombe la Shirikisho Tanzania Bara waliyocheza dhidi ya Coastal Union Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam suala lililoonyesha moja kwa moja kuwa kunajambo ambalo lipo ndani ya timu na kuifanya timu kuwa hivyo.

Pope amesema, anaamini kunawatu wanawashika wachezaji ili wacheze chini ya kiwango na matokeo yake wanashindwa kushindwa mechi mbalimbali hivyo wanalifanyia uchunguzi jambo hilo ili kujua ni watu gani na wanafanya hivyo kwa sababu gani.

Pope amesema, ilionekana dhahiri wanauwezo wa kuchukua ubingwa wa msimu huu lakini walipofika katika hatua nzuri ya kuwania ubingwa wa msimu huu ndipo pale kiwango cha baadhi ya wachezaji kilipoanza kushuka.

Pope amesema, kwenye siasa za Simba na Yanga fujo huanza pale mashabiki wanapotaka kumtoa kiongozi na uongozi ukishatoka huwa wanakuwa na mtu wao wanataka aingie.

Pope amesema, fujo za safari hii zimeandaliwa kabisa na baadhi ya watu kwani imefikia hatua mpaka baadhi ya wachezaji kupiga wachezaji wenzao kwa sababu wanajua kilichofanyika katika mchezo dhidi ya Toto ambapo Simba ilipoteza kwa bao 1-0 Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Pope amesema, mashabiki wanatakiwa kuangalia timu na wachezaji wanachokifanya na sio kushambulia viongozi kwani wachezaji ndio chanzo na kama wangewafuata na kuwaambia wangeweza kubadilika katika mechi zinazofuata.

Kwa upande mwingine Hans Pope amesema, kwa upande wa wachezaji kugoma wakishinikiza kulipwa mishahara yao sio sahihi kwani wanajua kabisa muda wa kulipwa mshahara ni kati ya tarehe tano au 10 sasa suala la kugoma kati ya tarehe sita na saba inaonekana ni msukumo kabisa.

Pope amesema, mshahara mara zote inatoka kwa wadhamini kwani wadhamini watatoa pesa wiki ya kwanza ya mwisho wa mwezi au wiki ya pili hivyo inaonekana kugoma kwa wachezaji ni shinikizo kutoka kwa baadhi ya mashabiki ambao hawana nia nzuri na timu hiyo.

Pope amesema, msimu huu walikuwa na timu bora kuliko misimu yote ambayo ineweza kuchukua Ubingwa lakini anaamini mashabiki wasio na nia nzuri na timu ndio chanzo cha kuiharibu timu mpaka imefikia hatua iliyopo sasa.

Simba imesaliwa na michezo miwili ikiwa na pointi 59 huku ikiendelea kushika nafasi ya tatu katika msimamo wa Ligi Kuu ya Soka Tanzania Bara.

JUKWAA LA KIMATAIFA LA KIUCHUMI KWAAJILI YA AFRIKA LIMEANZA RWANDA.

Jukwaa la kimataifa la 26 la uchumi kwa ajili ya Afrika limeanza mjini Kigali, mji mkuu wa Rwanda. Jukwaa hilo la siku tatu linawashirikisha washiriki karibu 1200 kutoka nchi 70 za dunia chini ya kauli mbiu ya 'Uunganishaji wa Vyanzo vya Afrika Kupitia Mageuzi ya Dijitali.'

Jukwaa hilo limeandaliwa katika hali ambayo bei ya malighafi imepungua sana kwa kadiri kwamba kuna ulazima wa kuanzishwa uchumi wa pande kadhaa katika upeo mzima wa uchumi wa bara la Afrika. Oliver Cann, msemaji wa jukwaa hilo huku akiashiria kuwa hali ya hivi sasa ya uchumi wa Afrika si kama ilivyokuwa katika miaka iliyopita amesisitiza kwamba hivi sasa kuna ufahamu mzuri kuhusiana na ulazima wa kuwepo uchumi wa pande kadhaa barani humo kwa lengo la kuzistawisha kiuchumi nchi za bara hilo.

Lengo la kupatikana uchumi kama huo ni kuziwezesha nchi hizo kutotegemea tu malighafi katika kuendesha uchumi wao. Amesema lengo jingine la kufanyika kikao hicho ni kuainishwa mbinu za ustawi wa baadaye kwa kutegemea teknolojia ya kisasa. Jukwaa la kimataifa la uchumi hufanyika kila mwaka huko Davos Uswisi likiwashirikisha viongozi wa kisiasa na kiuchumi kutoka pembe mbalimbali za dunia.

Jukwaa la kimataifa la uchumi kwa ajili ya Afrika pia kufikia sasa limefanyika katika nchi tofauti za bara hilo kwa lengo la kuchunguza njia mbalimbali za kuimarisha uchumi wa bara la Afrika ambao una mchango mdogo wa asilimia 3 tu katika uchaumi wa dunia. Inaonekana kuwa hivi sasa wawekezaji na wanauchumi wameamua kutumia teknolojia ya kisasa kwa ajili ya kuleta mageuzi makubwa katika uchumi wa Afrika.

Wakati huohuo wataalamu wa Mfuko wa Kimataifa wa Fedha IMF walitabiri mwezi Aprili uliopita kwamba uchumi wa nchi za Afrika zilizoko kusini mwa jangwa la Sahara ulipungua kasi kwa asilimia 3 mwaka uliopita. Kupungua kwa bei ya mafuta kuliacha athari kubwa katika uchumi wa nchi zinazouza nje mafuta za bara hilo kama Nigeria na Angola, na hivyo kuchangia katika kupungua kwa uchumi wa bara hilo.

Wakati huohuo kupungua kwa bei ya mafuta katika masoko ya kimataifa hakujakuwa na athari kubwa katika uchumi wa nchi zinazoagiza bidhaa hiyo muhimu barani humo. Hii ni katika hali ambayo asilimia 95 ya pato la serikali ya Angola linatokana na uuzaji wa mafuta.

Mdororo katika uchumi wa Uchina na vilevile hali ngumu ya kiuchumi duniani ni jambo ambalo limepelekea nchi nyingi za bara la Afrika kukabiliwa na nakisi ya bejeti.

Afrika Kusini ambayo inahesabiwa kuwa moja ya nchi zenye uchumi mkubwa zaidi barani Afrika pia inakabiliwa na hali ngumu ya uchumi ambapo uchumi wake unatathminiwa kukuwa kwa asilimia ndogo sana mwaka huu. Mivutano ya kisiasa na upinzani dhidi ya Rais Jacob Zuma wa nchi hiyo ni jambo ambalo linashirikiana na ukame na vilevile kupungua thamani ya sarafu ya taifa katika kupunguza ustawi wa uchumi wa nchi hiyo.

Mabadiliko ya hali ya hewa yanayosababishwa na Elnino yamevuruga pakubwa sekta za kilimo katika nchi za mashariki na kusini mwa bara la Afrika, zikiwemo za Afrika Kusini, Zambia, Zimbabwe na Malawi. Kupungua kwa mazao ya kilimo nchini Zimbabwe na bei ya shaba katika soko la kimataifa ni masuala muhimu ambayo yameathiri uchumi wa nchi hiyo na Zambia ambayo huzalisha kiwango kikubwa cha shaba duniani.

Katika eneo la mashariki mwa Afrika ukame umeathiri sana Ethiopia kwa kiwango ambacho kilikuwa hakijawahi kushuhudiwa katika miongo kadhaa iliyopita. Ni kwa kuzingatia suala hilo ndipo wataalamu wa IMF wakatabiri kwamba uchumi wa nchi hiyo utapungua kutoka asilimia 10 mwaka uliopita hadi asilimia 4.5 mwaka huu.

WHO: %80 YA WAKAZI WA MJINI WANAVUTA HEWA CHAFU.

Ripoti mpya iliyotolewa na Shirika la Afya Duniani (WHO) imeonya kuwa hali ya uchafuzi wa hewa inazidi kuwa mbaya duniani kote huku zaidi ya asilimia 80 ya wakaazi wa miji mikubwa wakivuta hewa chafu na kuongeza hatari ya kupatwa na saratani ya mapafu na maradhi mengine hatari.

Ripoti hiyo ya WHO imebainisha kuwa wakaazi wa mijini katika nchi masikini ndio wanaoathiriwa zaidi na kufafanua kwamba ni asilimia mbili tu ya miji katika nchi za kipato cha chini na cha kati ambayo watu wake wanavuta hewa inayokidhi viwango vya shirika hilo la kimataifa la afya. Kiwango hicho ni asilimia 44 katika miji ya nchi tajiri.

Ripoti ya Shirika Afya Duniani imezingatia utafiti iliofanya katika miji 795 ya nchi 67 katika kipindi cha kati ya mwaka 2008 hadi 2015.

Kwa kuzingatia kiwango cha mada zenye madhara kama sulfeti na kaboni nyeusi, WHO imegundua kuwa hewa inachafuka zaidi katika maeneo ya nchi zinazoendelea hususan katika Mashariki ya Kati na Kusini Mashariki mwa Asia.

Utafiti huo wa shirika la Afya Duniani umeonesha kuwa India ina miji 15 kati ya 30 duniani yenye hewa chafu zaidi.

Mji wa Zabol ulioko mashariki mwa Iran ndio wenye hewa chafu zaidi ukifuatiwa na miji ya Gwalior na Allahabad ya India na Riyadh na Jubail ya Saudi Arabia

MUUAJI WA MTU MWEUSI APIGA MNADA SILAHA YAKE.

George Zimmerman, muuaji wa Trayvon Martin, kijana wa Kimarekani mwenye asili ya Kiafrika ametangaza kuwa anaipiga mnada kwenye mtandao wa intaneti silaha aliyomuulia kijana huyo.

Zimmerman, mlinzi wa kizungu ambaye tarehe 16 Februari mwaka 2012 alimpiga risasi na kumuua Trayvon Martin pasina kuwa na silaha yoyote na kisha akafutiwa shtaka hilo hivi sasa ameamua kuipiga mnada silaha yake hiyo.

Kwa mujibu wa Zimmerman mwenyewe, silaha hiyo amerejeshewa na Wizara ya Sheria ya Marekani ambayo iliichukua kutoka kwake wakati kesi yake ilipokuwa ikiendelea na baada ya kufutiwa mashtaka.

Mnada wa kuiuza silaha hiyo umeanza jana Alhamisi na bei ya kuanzia imetajwa kuwa ni dola elfu tano.

Mauaji ya Trayvon Martin ambaye wakati huo alikuwa na umri wa miaka 17 na hatimaye kufutiwa mashtaka George Zimmerman kulizusha wimbi kubwa la machafuko na malalamiko katika kila pembe ya Marekani; na maandamano makubwa yakafanyika nchini humo na katika baadhi ya nchi za kigeni kulalamikia ubaguzi dhidi ya Wamarekani wenye asili ya Kiafrika.

SOMALIA YAKOSOA MPANGO WA KENYA KUFUNGA KAMBI ZA DADAAB.

Serikali ya Somalia imekosoa azma ya Kenya ya kufunga kambi ya wakimbizi ya Dadaab yenye mamia ya maelfu ya wakimbizi na haswa raia wa Kisomali.

Taarifa ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Somalia imesema kufungwa kwa kambi hiyo hakutakua na tija nyingine ghairi ya kuwasukuma wakimbizi hao kujiunga na makundi ya kigaidi kama vile al-Shabab. Taarifa hiyo imeongeza kuwa, kuwatimua wakimbizi hao wakati huu ambapo nchi hiyo ya Pembe ya Afrika iko mbioni kuhakikisha kuwa inarejesha usalama, uthabiti na kuimarisha taasisi zake, kutayumbisha zaidi usalama wa kanda hiyo. Kambi ya Dadaab ina wakimbizi wapatao 350,000, aghalabu yao wakiwa ni raia wa Kisomali.

Haya yanajiri siku chache baada ya Umoja wa Mataifa kuitaka serikali ya Kenya kufikiria upya mpango wake wa kufunga kambi hiyo huku ukisisitza kuwa, usalama wa maelfu ya wakimbizi wa Kisomali na raia wa Sudan Kusini kwa takriban robo karne umekuwa ukitegemea ukarimu wa Kenya na nia yake ya kutaka kuonyesha mfano bora katika eneo wa kutekeleza wajibu wake wa kimataifa. Hii ni katika hali ambayo, Shirika la Madaktari Wasio na Mipaka MSF nalo limetoa taarifa likisema kuwa, kutekelezwa kwa uamuzi huo kutawaweka maelfu ya wakimbizi hatarini. Licha ya mashirika mbalimbali ya kimataifa kuendelea kuitaka Kenya ifikirie upya uamuzi wake wa kutaka kufunga kambi ya wakimbizi ya Dadaab, serikali ya Nairobi imesisitiza kwamba, inalazimika kuifunga kambi hiyo ya wakimbizi kutokana na mzigo mzito wa kiusalama, kiuchumi na masuala ya kimazingira.

UN YAITAKA SUDAN KUSINI KUFUATILIA JINAI ZA NGONO.

Mwakilishi Maalumu wa Umoja wa Mataifa anayeshughulikia Ukatili wa Kingono Katika Migogoro ameutaka uongozi mkuu wa serikali ya mpito ya umoja wa kitaifa ya Sudan Kusini utekeleze ahadi ulizotoa za kufuatilia jinai za ukatili wa kingono zilizofanywa nchini humo.

Akikamilisha safari yake ya siku nne mjini Juba hapo jana, Zainab Hawa Bangura, ameeleza mbele ya waandishi wa habari kuwa kutekelezwa kwa mafanikio makubaliano ya amani kutahitaji kuhakikisha kuwa jinai za ukatili wa kingono zinafuatiliwa, kufahamika na kuripotiwa na kushughulikiwa katika vyombo vyote vya sheria vya serikali ya mpito.

Mwakilishi huyo Maalumu wa Umoja wa Mataifa anayeshughulikia Ukatili wa Kingono Katika Migogoro amebainisha kuwa ahadi hizo zimo kwenye taarifa ya pamoja ambayo waliisaini yeye na Rais Salva Kiir Oktoba 11 mwaka 2014 na pia kwenye taarifa ya upande mmoja iliyotolewa Desemba 18 mwaka 2014 na Makamu wa Kwanza wa Rais wa hivi sasa wa nchi hiyo Riek Machar.

Bi Bangura amesisitiza kuwa licha ya ahadi hizo na hatua zilizopigwa katika utekelezaji lakini jinai za ukatili wa kingono zimeendelea kufanywa katika muktadha wa mgogoro wa nchi hiyo.

Katika safari yake ya siku nne nchini Sudan Kusini iliyotokana na mwaliko wa serikali ya Juba, Mwakilishi Maalumu wa Umoja wa Mataifa anayeshughulikia Ukatili wa Kingono Katika Migogoro amekutana na kufanya mazungumzo na Rais Salva Kiir, Makamu wa Kwanza wa Rais Riek Machar na maafisa wengine wa ngazi za juu wa serikali ya mpito ya umoja wa kitaifa ya nchi hiyo. Bi Zainab Hawa Bangura amefanya mazungumzo pia na makundi ya wanawake yanayotoa huduma kwa manusura wa ukatili wa kingono, jumuiya ya utoaji huduma za kibinadamu na jopo la wanadiplomasia walioko nchini humo.

IRAN HAITAPELEKA MAHUJAJI WAKE SAIDIA MWAKA HUU.

Waziri wa Utamaduni na Miongozi ya Kiislamu wa Iran amesema, viongozi wa Saudi Arabia wanaendelea kukwamisha juhudi za Waislamu wa Iran za kwenda kutekeleza amali ya Hija mwaka huu.

Ali Jannati amesema hayo leo Alkhamisi wakati alipoonana na Ayatullah Sayyid Abdul Karim Mousavi Ardebili, mmoja wa maulamaa wakubwa na marjaa taqlidi wa mjini Qum, kusini mwa Tehran na kuongeza kuwa, takriban miezi minne imepita sasa tangu Iran ianze juhudi za kufuatilia namna wananchi wake watakavyokwenda kutekeleza amali ya Hija mwaka huu, lakini viongozi wa Saudia wanaendelea kukataa mapendekezo ya Iran katika masuala kama vile viza, usafiri wa anga na kudhaminiwa usalama wa mahujaji wa Iran, hasa kutokana na kuwa hakuna ubalozi wa Saudia nchini Iran.

Waziri wa Utamaduni na Miongozo ya Kiislamu wa Iran amesema, hadi hivi sasa viongozi wa Saudia hawajatoa ahadi zozote kuhusiana na suala la viza bali wanachotaka wao ni mahujaji wa Iran kwenda kuomba viza nchi nyingine, suala ambalo linaonesha wazi kuwa mazingira ya kuweza Waislamu wa Iran kwenda kutekeleza ibada ya Hija mwaka huu hayapo.

Waziri wa Utamaduni na Miongozo ya Kiislamu wa Iran ameelekea mjini Qum kwa ajili ya kuonana na marajii na maulamaa wakubwa wa kidini mjini humo.

MASHINDANO YA QURAN YAANZA LEO IRAN.

Baada ya Dk Ali Larijani, Spika wa Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu (Bunge la Iran) kufungua duru ya 33 ya mashindano ya kimataifa ya Qur'ani Tukufu jana Jumatano, mashindano hayo yameanza rasmi leo.

Mashindano hayo yameanza kwa kuchuanishwa washindanaji wa kuhifadhi Qur'ani nzima na qiraa na uhakiki wa Qur'ani.

Shirika la habari la IQNA limeripoti kuwa, mashindano ya qiraa na kuhifadhi Qur'ani nzima yamefanyika katika kumbi za hoteli walizofikia washindanaji hao mbele ya majaji wa kimataifa ikiwa ni hatua ya mchujo wa kuchagua watu wa kuingia kwenye ukumbi mkuu wa mashindano.

Itakumbukwa kuwa nchi 75 zina wawakilishi wao katika mashindano hayo. Hayo yamesemwa na Sheikh Ali Mohammadi Mwakilishi wa Faqihi Mtawala na Mkuu wa Taasisi ya Wakfu ya Iran ambaye ameongeza kwamba, kutakuwa na washiriki 130 kutoka nchi 75 katika mashindano hayo.

Amesema kwa mara ya kwanza mashindano hayo yanafanyika katika Ukumbi Mkubwa wa Swala wa Imam Khomeini MA hapa jijini Tehran, ili kuwezesha idadi kubwa ya watu kujumuika katika mashindano hayo.

Sheikh Ali Mohammadi ameongeza kuwa, mashindano ya mwaka huu yatakuwa na washiriki kutoka mabara ya Afrika, Asia, Ulaya, Marekani na Pasifiki.

Mashindano hayo ya Kimataifa ya Qur'ani Tukufu yanatarajiwa kumalizika siku ya Jumanne ya mwezi kumi Shaaban, sawa na tarehe 17 mwezi huu wa Mei.

MSEVEN AAPISHWA KUWA RAIS KWA KIPINDI CHA TANO MFULULIZO.

Rais Yoweri Museveni wa Uganda ambaye lishinda katika uchaguzi wa mwezi Februari mwaka huu, leo Alkhamisi ameapishwa kuwa rais wa nchi hiyo kwa kipindi cha tano mfululizo.

Sherehe za kuapishwa Yoweri Museveni ambazo zimefanyika jijini Kampala, zimehuhudhuriwa na marais wa nchi kadhaa za Afrika akiwemo Rais Omar al Bashir wa Sudan.

Museveni (71) aliingia madarakani mwaka 1986 nchini Uganda na katika uchaguzi wa tarehe 18 Februari mwaka huu, ameshinda kwa asilimia 60.62 ya kura.

Wasimamiaji wa kimataifa wamesema kuwa uchaguzi wa Rais nchini Uganda ulifanyika katika anga ya vitisho na hofu iliyosababishwa na miamala mibaya ya serikali.

Daktari Kizza Besigye, mmoja wa wagombea wa upinzani amekataa matokeo hayo na kujitangaza mshindi.

Jana polisi wa Uganda walimtia mbaroni Dakta Besigye. Baada ya kukamatwa Besigye, chama chake cha FDC kilisambaza mikanda ya video katika mitandao ya kijamii, inayoonyesha kiongozi wao huyo akiapishwa kama rais wa Uganda na kusema kuwa kiapo cha leo cha Rais Museveni si halali.

SIMBA: YANGA NA NDANDA KUCHEZA TAIFA NI RUSHWA.

Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano Jerry Muro amesema, Ndanda FC itakapoutumia Uwanja wa Taifa itamaanisha kwamba Ndanda FC watakuwa nyumbani na hata mapato katika mgao asilimia kubwa ataipata Ndanda hivyo haoni sababu ya wengine kuanza kuongea kwa kuona ni makosa katika mchezo huo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Klabu ya Simba Zacharia Hans Pope amesema, mchezo huo ni sio halali kwani inaonekana ni rushwa ya waziwazi kwa timu hizo, kwani haiwezekani umfadhili mpinzani wako ambaye unashindana na ukategemea matokeo ya halali.

Yanga ambayo ndio bingwa wa Ligi Kuu ya Soka Tanzania Bara msimu wa 2015/16 wakiwa wamesalia mechi mbili mkononi itakutana na Ndanda F Jumamosi Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam ambapo mara baada ya kukamilika kwa mchezo huo, Yanga watakabidhiwa Kombe la Ubingwa wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara.

MSUKUMA HABARI YAKO.


1
Mpemba sabalheri, unaionaje hali,
Kwangu mie ni buheri, namshukuru Jalali,
Usiwe na munkari, lijibu langu suali,
Kwanini wapenda shari, kama vile hauswali?
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
2
Mgogo habari yako, salamu zangu pokea,
Hapa nina swali lako, lile ulilo zoea,
Kuomba silika yako? jibu ninalingojea,
Lini unarudi kwako? Dom ulipotokea?
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
3
Mtumbatu nampenda, wenzangu naweka wazi,
Mtu huyu hana inda, tena hana utalazi,
Mwaminifu kama kunda, akiwa na laazizi,
Sishangae akikonda, sababu ya mkumbazi.
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
4
Mmakunduchi mpole, si mwepesi kuchukia,
Tena hapendi kelele, na fujo kuzisikia,
Aenda huku na kule, kuti ajitafutia,
Ila mvivu kwa shule, umande aukimbia,
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
5
Mzaramo sikupati, zinduka silale doro,
Uwate tupu kibeti, isifike yako soro,
Wapenda kichenipati, watoto wakosa karo,
Unalitunza kabati, nguo waweka kwa poro,
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
6
Msukuma simsemi, ila ukweli nampa,
Sio kwamba hajitumi, tatizo ni zake pupa,
Pombe ageuza maji, huku nguo azitupa,
Akifika kwenye lami, anayavua malapa.
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
7
Mnyakyusa kwa vioja, hakuna wa kumpata,
Fulusi anazifuja, kama vile aokota,
Aagizia mapaja, jikoni yalo tokota,
Anywa supu kwa mrija,soda kwake tarumbeta,
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
8
Mhaya apenda sifa, tena kupita kiasi,
Aweza lalia fafa, kibanda chake cha nyasi,
Pia asiwe na sofa, masikini si mkwasi,
Atatamba sio lofa, ana kasri Parisi
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
9
Mhehe si mchokoze, hasa yule wa Kalenga,
Tena simgombeze, usimfanyie ngenga,
Hujui na nikujuze, mwepesi wa kujinyonga,
Kosa lake mueleze, maneno ukiyachunga.
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
10
Mkuriya ana nini, leo nataka ukweli,
Kila siku gazetini, mara lile mara hili,
Kumwaga damu mwilini, kwake yeye ni sahali,
Ana tatizo rasini, kiasi aitwe nduli,
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
11
Mluguru kwa kulima, mwenzenu nampongeza,
Gimbimaji na mlima, kuchemsha anaweza,
Wali wake kama sima, wallahi hutaongeza,
Atasema kwa heshima, mkono umeteleza,
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
12
Mchaga toka Machame, aongoza ubahili,
Yu tayari akuchome, kikubwa apate dili,
Asemwa ni gumegume, ati ni yake asili,
Kama mate umteme, kiumbe huyu katili,
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
13
Mha atege sikio, nisemalo asikie,
Anajua kwenda mbio, lengo lake litimie,
Afanye watu fagio, njia wamsafishie
Apate mafanikio, awaacha wajifie.
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
14
Mkwere ana maneno, huyasema rejareja,
Kwa mithali na mifano, huzichanganya lahaja,
Kesha maliza matano, weye huna hata moja,
Vile bila ndoano, ajipatia kangaja,
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
15
Mnyamwezi kwa ushamba, nadhani atia fora,
Avae apige pamba, utacheka kama jura,
Akiwa alima shamba, anaruka kama chura,
BASATA wakimbamba, 'taungana na Snura.
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
16
Mdigo yule wa Tanga, asifika kwa kupika,
Uchungu wote wa chunga, kirahisi inalika,
Kwa mapenzi ndio nanga, ukizama hutatoka,
Ukikutoka ujinga, nguo anaziloweka,
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
17
Mpare wa milimani, analima tangawizi,
Anashangaza jamani, chai yake ya mluzi,
Haipiki na majani, yaani hata mizizi,
Wanayo fikira gani, mjue sijamaizi,
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
18
Mfipa kwake Mpanda, Mpimbwe na Sumbawanga,
Kibeku anakipanda, anapaa akiwanga,
Hufanya analopenda, kwa tunguri na usinga,
Akitaka kukuwinda, anakuchinjia ninga.
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
19
Mmakonde mla panya, ati samaki mchanga,
Leo mimi nakukanya, ndugu yangu wa Nambunga,
Hebu jaribu kufanya, uvue japo mkunga,
Rohoni nimekusinya, natamani kukutenga.
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.
20.
Kaditama samahani, nyie nilio wakwaza,
Mimi ni wenu mtani, sio yule wa Vigwaza,
Natokea undambani, Ifakara si Muheza,
Msiweke mtimani, lengo si kuwachokoza.
Nang'ata na kupuliza, utani nawatania.

Dotto Rangimoto Chamchua(Njano5)
whatspp/call 0622845394 Morogoro.

NINI MAANA YA UKIMYA WA JOHN MNYIKA??

Na Charles Francis M,

Kwa muda mrefu sasa naibu katibu mkuu wa Chadema bara, ambaye pia ni mbunge wa jimbo la Kibamba, ndugu John Mnyika amekuwa kimya katika majukwaa ya kisiasa. Mnyika kwa nafasi yake kama naibu katibu mkuu wa chama kikuu cha upinzani, lakini pia kwa nafasi yake ya ubunge na "mtindo" wake wa kuibua hoja na kueleza bila kuogopa, hakustahili kuwa kimya!

Kimya hiki kimeibua hoja nyingi sana lakini hoja kuu nne zimekuwa zikijadiliwa sehemu mbali mbali. Hoja hizi zinaonekana kila moja kwa nafasi yake kubeba aina fulani ya ukweli. Hoja hizi ni pamoja na:

1. UJIO WA LOWASSA NA AGENDA YA UFISADI.

Ikumbukwe kwamba wakati wa mchakato wa kumpata mgombea Urais ndani ya chama cha Chadema, mpasuko mkubwa ulitokea mara baada ya Lowassa kujiunga na Chadema na kupewa ridhaa ya kuwa mgombea wa Urais. Ina aminika kwamba baada ya Lowassa kuingia Chadema ile agenda ya Ufisadi "ikazikwa" rasmi maana agenda ile kwa kiasi kikubwa ilimlenga Lowassa, hivyo kuhamia kwake kukawa pigo na mpasuko kwa Chadema.

Hali inaonekana kumkera John Mnyika na hivyo kuamua kutozungumzia suala lolote linalo husu chama au Lowassa mwenyewe. Ikumbukwe pia tangu Lowassa ajiunge na Chadema, ni naibu katibu mkuu (Zanzibar) pekee ambaye amekuwa akizungumzia ujio wa Lowassa na siyo Mnyika kama ambavyo "protocol" ya uongozi ilitaka! Ujio wa Lowassa unaonekana kukifanya chama hicho kipoe na kikose agenda mbadala ya kusimamia ikilinganishwa na kasi ya serikali ya sasa.

2. AFYA YA JOHN MNYIKA.

Kundi la pili wana hoja kwamba kwa sasa John Mnyika inawezekana akawa ni mgonjwa na hivyo kukosa muda wa kuwa majukwaani au kuonekana katika medani za kisiasa kama ilivyo zoeleka! Suala hili haliko wazi sana, siyo chama wala Mnyika mwenyewe walio zungumza juu ya suala hili.

3. MIPANGO NA MIKAKATI YA "SIRI".
Kuna kundi lingine wana imani kwamba ukimya wa John Mnyika ni mkakati wake wa "siri" ili aibuke na hoja nzito ya kitaifa kukinusuru chama chake au ni mkakati wake binafsi wa kujijenga kisiasa na kuondoa aina ya siasa hasa za chama chake ambazo zimekuwa zikitafsiriwa kama siasa za "vurugu" "mihemko" na matukio!

4. CHAMA KUENDESHWA "NDIVYO SIVYO"
Kundi lingine lina amini kwamba John Mnyika hapendezwi na mwenendo wa chama chake kuwa kama mali ya watu wachache. Kundi hili wana amini kwamba Chadema ina endeshwa na watu wachache ambao maamuzi yao hayapingwi na ukipinga unaitwa "MSALITI". Watu wa kundi hili wana amini kwamba Chadema ya sasa haina mashiko, inapoteza mwelekeo na kujisahihisha kwake ni vigumu kwa mfumo huu wa maamuzi ya watu wachache na "hasa mwenyekiti". Kundi hili wana amini pia siasa za "harakati" zimekwisha poteza mwelekeo, kwa sasa ni siasa za "utendaji".

Ukimya wa John Mnyika bado ni kitendawili kwa wengi, ukimya wake unataka kufanana na ule alio anza kuonyesha Dk Slaa kipindi cha uchaguzi mpaka alipo tangaza kujiondoa Chadema. Wapo wanao amini kwamba Mnyika anataka kufanya "maamuzi" MAGUMU.

Haya yote yanabaki kuwa nadharia tu, ni maoni na mawazo ya watu! Ukweli anao John Mnyika mwenyewe, je wewe unaona mtazamo gani kati ya hii ni sahihi??

"Caytano Maytano"

Charles Francis M.