RWANDA YAKANUSHA KUHUSIKA NA MACHAFUKO YANAYO ENDELEA BURUNDI.

Serikali ya Rwanda imetoa ufafanuzi kuhusiana na tuhuma dhidi yake kwamba, imekuwa ikichochea machafuko katika nchi jirani ya burundi.

Rais Paul Kagame wa Rwanda amekanusha madai dhidi ya nchi yake kwamba, inawasaidia waasi wa Burundi kama ilivyokuja katika ripoti ya siri iliyowasilishwa kwa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.

Rais Kagame amesisitiza kuwa, nchi yake haiwasaidii kwa namna yoyote ile waasi wa Burundi au kuhusika na machafuko yanayoendelea kushuhudiwa katika nchi hiyo jirani. Rais Kagame amebainisha kwamba, machafuko ya ndani nchini Burundi chimbuko lake ni masuala ya ndani ya nchi hiyo.

Imeelezwa katika ripoti ya siri iliyowasilishwa kwa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kwamba, Rwanda imekuwa ikiwasaidia waasi wa Burundi wanaotaka kuiangusha serikali ya Rais Pierre Nkurunziza.

Ripoti hiyo ya wataalamu wa Umoja wa Mataifa inaeleza kwamba, Rwanda imekuwa ikiwasaidia kifedha, kimafunzo na hata kilojistiki waasi hao wanaopigana dhidi ya serikali ya Bujumbura.

Imeelezwa kuwa, Rwanda inafanya hivyo ili kuiondoa madarakani serikali ya Rais Nkurunziza.

Lambert Mende Omalanga ambaye ni msemaji wa serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo pia anaamini kuwa, serikali ya Rwanda imewapatia fedha waasi wa Rais Joseph Kabila ili kuwaimarisha.

Mende Omalanga amesema kuwa, Rwanda imekuwa ikiwapatia fedha wanachama wa kundi la zamani la waasi wa M23 ambao walisambaratishwa Novemba mwaka 2013 na kwa sasa baadhi yao wanaishi uhamishoni katika nchi za Rwanda na Uganda.

Ripoti ya siri ya wataalamu wa Umoja wa Mataifa iliyopelekwa katika Baraza la Usalama imefichua kwamba, waasi wa Burundi walioko mashariki mwa DRC wamekiri kwamba, katikati mwa mwaka jana walipatiwa mafunzo na watoaji mafunzo ambao baadhi yao walikuwa ni wanajeshi wa Rwanda.

Ripoti hiyo ya wataalamu wa Umoja wa Mataifa inakinzana na matamshi ya hivi karibuni ya viongozi wa Magharibi. Viongozi hao walidai kwamba, serikali ya Rwanda ilisimamisha himaya yake kwa waasi wa Burundi tangu mwaka jana.

Wataalamu wa Umoja wa Mataifa wanasema kuwa, wameipatia serikali ya Rwanda ushahidi unaoonesha juu ya kuweko ushirikiano wa siri kati yake na waasi wa Burundi na wa Congo DR. Aidha serikali ya Burundi ikishirikiana na jirani yake Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo imesema kuwa, ina nyaraka zinaoonesha juu ya kuweko harakati za siri za Shirika la Kiintelijensia la Rwanda. Pamoja na hayo serikali ya Rwanda imeendelea kukana kuhusika kwa namna yoyote ile na machafuko ya jirani yake Burundi.

Burundi ilitumbukia katika rangaito na mchafukoge Aprili mwaka 2015 baada ya Rais Pierre Nkurunziza kuidhinishwa na chama chake cha CNDD-FDD kuwania kiti cha Urais kwa mara ya tatu mfululizo.

Licha ya kuweko upinzani wa asasi za kiraia nchini Burundi na hata za kieneo na kimataifa, Nkurunziza alishiriki katika uchaguzi huo na kuibuka na ushindi na hivyo kushika hatamu za uongozi wa nchi hiyo kwa mara ya tatu mfululizo.

Kuendelea upinzani na maandamano kuliibua machafuko katika jiji la Bujumbura na miji mingine mikubwa ya nchi hiyo.

Takwimu zinaonesha kuwa, watu 500 wameuawa na wengine karibu laki mbili na 60 elfu wamekuwa wakimbizi tangu nchi hiyo ilipotumbukia katika machafuko hayo.

Katika kipindi chote hiki tangu Burundi itumbukie katika mgogoro wa kisiasa, wachambuzi wa masuala ya kisiasa wamekuwa wakitoa indhari mara chungu nzima juu ya hatari ya nchi hiyo kutumbukia katika vita vya ndani na vya mauaji ya kimbari.

Katika mazingira kama haya ya kutia wasiwasi, himaya ya kifedha na kijeshi kwa makundi yanayofanya fujo nchini Burundi au katika nchi jirani ni sawa na kumwagia mafuta ya petroli moto unaowaka.

AMNESTY YATAKA UGANDA IMKAMATE RAIS OMAR AL BASHIR.


Mashirika ya kimataifa ya kutetea haki za binadamu yameitaka serikali ya Uganda kumkamata Rais Omar al-Bashir wa Sudan na kumkabidhi kwa Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ICC, kwa tuhuma za mauaji ya kimbari katika eneo la Darfur na jinai dhidi ya binadamu.

Mashirika ya kutetea haki za binadamu ya Amnesty International na Human Rights Watch yameitaka serikali ya Uganda kutekeleza wajibu wake wa kimataifa na kumkabidhi kwa mahakama ya ICC, Rais wa Sudan ambaye alienda mjini Kampala kuhudhuria hafla ya kuapishwa Rais Yoweri Museveni.

Muthoni Wanyeki, Mkurugenzi wa Amnesty International katika kanda ya Afrika Mashariki, Pembe ya Afrika na eneo la Maziwa Makuu amesema Uganda ni mwanachama wa Mkataba wa Roma uliobuni Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ICC na hivyo, iwapo itafeli kumkabidhi Rais wa Sudan, itakuwa imeshindwa kutekeleza wajibu wake wa kimataifa. Hii ni katika hali ambayo, baada ya kula kiapo hapo jana, Rais Museveni aliikashifu ICC na kusema kuwa mahakama hiyo imegeuka na kuwa chombo cha kuwadhalilisha viongozi wa Kiafrika huku ikiwasaza viongozi makatili wa nchi za Magharibi. Kauli ya Museveni iliwaghadhabisha wajumbe wa Marekani na Umoja wa Ulaya waliokuwa wamehudhuria sherehe za kuapishwa kwake katika Viwanja vya Kololo jijini Kampala na kuwafanya kuondoka kwenye hafla hiyo.

Itakumbukwa kuwa, serikali ya Afrika Kusini ilikataa kumkamata Rais Omar al-Bashir ambaye alishiriki mkutano wa viongozi wa Afrika uliofanyika mjini Johannesburg Julai mwaka jana. Aidha Kenya ilipuuza wito wa kumkamata na kumkabidhi kiongozi huyo kwa Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai ICC anakotakiwa kujibu tuhuma za mauaji ya kimbari katika eneo la Darfur na jinai dhidi ya binadamu; alipohudhuria sherehe za kuapishwa Rais Uhuru Kenyatta wa nchi hiyo ya Afrika Mashariki mwaka 2013.

HIZBULLAH YACHUNGUZA KIFO CHA KAMANDA WAKE.


Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Lebanon ya Hizbullah imesema imeanzisha uchunguzi kubaini namna kamanda wake mwandamizi alivyouawa katika kile kilichotajwa kuwa hujuma ya jeshi la utawala wa Israel.

Taarifa ya Hizbullah imesema kuwa, harakati hiyo imeanzisha uchunguzi kubaini iwapo Mustafa Badruddin aliuawa katika hujuma ya anga ya jeshi la utawala wa Kizayuni wa Israel katika moja ya kambi za harakati hiyo karibu na uwanja wa ndege wa Damascus au la.

Taarifa hiyo imeongeza kuwa, uchunguzi wao unalenga kujua iwapo kamanda huyo mwandamizi aliuawa katika shambulizi la kombora au roketi, baada ya sauti kubwa ya kishindo kusikika jana katika kambi hiyo.

Ripoti za awali zilikua zimearifu kuwa Mustafa Badruddin, kamanda mwandamizi wa Hizbullah ya Lebanon aliuawa katika hujuma ya anga ya ndege ya utawala wa Israel.

Badruddin mwenye umri wa miaka 55 na ambaye alikua mkuu wa tawi la kijeshi la Harakati ya Kiislamu ya Lebanon Hizbullah, alikuwa akiongoza kikosi kinachoisaidia serikali ya Rais Bashar al-Assad wa Syria kupambana na makundi ya kigaidi katika nchi hiyo ya Kiarabu.

Kamanda huyo ambaye pia alikua mshauri wa Hassan Nasrullah, Katibu Mkuu wa Hizbullah na mkuu wa kitengo cha kiintelijensia, alikua binamu ya Imad Mughniyah, kamanda mwandamizi wa zamani wa Hizbullah ambaye aliuawa na kitengo cha ujasusi cha utawala wa Israe Mossad, mwaka 2008 katika mji mkuu wa Syria.

MAGAID WA DAESH WAUA WANAJESHI 17 WA IRAQ.


Takriban askari 17 wa jeshi la Iraq wameuawa katika shambulizi la bomu lililofanywa na kundi la kigaidi  la Daesh katika mkoa wa Anbar, magharibi mwa nchi hiyo.

Duru za kijeshi zinaarifu kuwa, magaidi hao jana Alkhamisi walilishambulia kwa mabomu gari la kijeshi katika wilaya ya Jarayshi, yapata kilomita 10 kutoka Ramadi, makao makuu ya mkoa wa Anbar na kuua askari 17 wa jeshi la serikali.

Imearifiwa kuwa, lengo la hujuma hiyo ya magaidi wa Daesh ni kukata mawasiliano kati ya eneo la Ramadi na Tharthar, lililoko kilomita 120 kaskazini magharibi mwa mji mkuu Baghdad ili kuwazuia wanajeshi wa Iraq kusonga mbele na kukomboa maeneo ambayo yanadhibitiwa na kundi hilo la kigaidi.

Aidha raia wawili waliuawa jana Alkhamisi katika hujuma tofauti ya kundi la kigaidi la Daesh katika eneo la al-Obeidi, mashariki mwa Baghdad.

Hujuma za jana zimefanyika siku moja baada ya magaidi hao kutekeleza shambulizi jingine lililosababisha makumi ya watu kupoteza maisha.

Siku ya Jumatano, watu wasiopungua 64 waliuawa na wengine zaidi ya 85 kujeruhiwa katika mripuko wa bomu uliotokea karibu na soko la Urayda katika kitongoji cha Sadr mashariki mwa mji mkuu wa Iraq, Baghdad.

RAIS WA GUINEA BISSAU AMFUTA KAZI WAZIRI MKUU.


Rais José Mário Vaz wa Guinea-Bissau amempiga kalamu Carlos Correia, Waziri Mkuu wa nchi hiyo na kutangaza kuivunja serikali.

Akilihutubia taifa jana Alkhamisi, Rais Vaz alisema serikali ya Correia imeshindwa kuupatia ufumbuzi mgogoro wa kisiasa uliopo na kubuni taasisi zinazoendana na matakwa ya utawala wake.

Rais José Mário Vaz wa Guinea-Bissau amevitaka vyama vya siasa kushauriana na kumteua Waziri Mkuu mpya.

Correia alipewa jukumu la kuwa Waziri Mkuu wa nchi hiyo ndogo ya magharibi mwa Afrika mwezi Oktoba mwaka jana, akiwa ni kiongozi wa tatu kushikilia wadhifa huo ndani ya muda wa miezi mitatu. Correia kama wenzake wawili waliomtangulia, alitazamiwa na utawala wa Rais Vaz kuupatia ufumbuzi mzozo wa kisiasa unaotokota nchini humo unaodaiwa kuripuka kuanzia ndani ya chama tawala cha PAIGC.

Mapema mwezi Machi mwaka huu, Ujumbe wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ulioitembelea nchi hiyo kwa ajili ya kuchunguza hali ya mambo, umeyasema hayo wakati wa mazungumzo na Rais wa Guinea-Bissau, José Mário Vaz, Spika wa Bunge na viongozi wa vyama vya kisiasa.

Mgogoro wa kisiasa nchini Guinea-Bissau umekuwa mkubwa kiasi cha kufanya upatanishi wa Jumuiya ya Uchumi ya Nchi za Magharibi mwa Afrika (ECOWAS) na Jumuiya ya Nchi Zinazozungumza Lugha ya Kireno (CPLP) kushindwa kumaliza mivutano hiyo ya kisiasa

KAMANDA WA HEZBOLLAH AMEUAWA.

Kundi la wapiganaji la Hezbollah limesema kuwa kamanda wake wa juu,Mustafa Badreddine ameuawa katika shambulio la anga la Israel nchini Syria,Vyombo vya habari vimeripoti.Mustafa Badreddine anadaiwa kuhusika na mauaji ya Waziri mkuu wa Israel Rafiq Hariri mwaka wa 2005.

VIRUS VYA EBOLA HUJIFICHA HUISHI KATIKA SHAHAWA.


Utafiti waonesha kuwa virusi vya Ebola vinaweza kuishi katika shahawa ya wagonjwa wanaopona kwa mwaka mzima

Taasisi ya Pasteur ya Ufaransa imetoa taarifa ikisema, utaifiti moja uliofanywa na watafiti wa Ufaransa na Guinea unaonesha kuwa virusi vya Ebola vinaweza kuishi katika shahawa (sperms) za wagonjwa wanaopona kwa mwaka mzima.

Utafiti huo unafanywa na taasisi ya Pasteur, Taasisi ya maendeleo ya Ufaransa, Taasisi ya afya na matibabu ya Ufaransa na mashirika ya utaifi ya Guinea. Matokeo ya utafiti huo yametolewa katika jarida la “Maradhi ya kuambukiza” la Marekani.
Watafiti waliwachunguza wagonjwa 450 wa Ebola waliopona kwa mwaka mazima, na kuchambua majimaji ya mwili wao, yakiwemo machozi, mate na shahawa.

Uchambuzi wa sampuli za shahawa 98 ya wagonjwa 68 waliopona unaonesha kuwa kufuatia ongezeko la uponaji wa wagonjwa hao, idadi ya virusi vya Ebola katika shahawa zao inapungua. Katika mwezi mmoja hadi mitatu baada ya kupona kwa wagonjwa, asilimia 28.5 ya shahawa ina virusi vya Ebola; Baada ya miezi 7 hadi 9, kiwango hicho kinapungua hadi asilimia 6.5; baada ya miezi 12, virusi vya Ebola vikatoweka katika shahawa.

Hivyo, watafiti wanapendekeza wagonjwa wa Ebola wanopona katika miezi kadhaa baada ya kupona wanatumia mpira wakati wa ngono, na kushauri masharika husika kufuatilia afya za wagonjwa hao, ili kuepuka maambukizi ya virusi hivyo kuibuka tena.

NEWCASTLE NA NORWICH ZIMESHUKA DARAJA.


Ushindi wa Sunderland wa 3-0 dhidi ya Everton Jumanne uliwafikisha hadi alama 38 na kwa kuwa Norwich na Newcastle hawawezi kuwafikia, moja kwa moja klabu hizo mbili zikashushwa daraja.

Kwa sasa Norwich wana alama 34 sawa na Newcastle. Klabu nyingine iliyoshushwa daraja ni Aston Villa iliyo na alama 17 kwa sasa.
Troy Deeney alikuwa amewapa Watford uongozi mechi hiyo iliyochezewa Carrow Road lakini Norwich wakajibu kupitia bao la Nathan Redmond.

Dieumerci Mbokani aliwafungia Norwich la pili naye Craig Cathcart akawaongezea la tatu kwa kujifunga.

Odion Ighalo alikomboa bao la pili lakini Mbokani akawafungia Norwich bao la nne.
Baada ya kushushwa daraja, Norwich sasa watakuwa wakichezea tu fahari mechi yao ya mwisho dhidi ya Everton Jumapili.

WA KIMATAIFA KUIFUATA ESPERANCA JUMAPILI.


Yanga itaondoka Dar es Salaam siku moja tu baada ya kukabidhiwa Kombe la ubingwa wa Ligi Kuu ya Soka Tanzania Bara katika mchezo dhidi ya Ndanda FC ya Mtwara Uwanja wa Taifa.

Bodi ya Ligi Kuu Tanzania Bara (TPLB) imeidhinisha mchezo Ndanda na Yanga kuchezwa Uwanja wa Taifa, badala ya Nangwanda Sijaona, Mtwara baada ya klabu hizo kukubaliana.

Yanga inatarajiwa kucheza na wapinzani wao, Sagrada Esperanca ya Angola kati ya Mei 17 au 18 mwaka huu Katika mchezo wa kwanza ulifanyika Dar es Salaam Jumamosi iliyopita ambapo Yanga iliwafunga wageni wake mabao 2-0 Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Yanga inahitaji ama sare, ushindi na kama kufungwa basi si zaidi ya bao moja ili kuindoa Esperanca katika hatua ya awali, ili kuingia hatua ya makundi katika kusonga mbele.

Wakati huo huo Rais wa Shirikisho la Soka nchini TFF Jamal Emil Malinzi ameipongeza Yanga kwa kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Soka Tanzania Bara kwa mara ya pili mfululizo baada ya kufanya hivyo msimu uliopita wa mwaka 2014/2015.

Hii ni mara ya 26 kwa Yanga kutwaa taji tangu kuanza kwa Ligi Kuu Tanzania Bara mwaka 1965, ikifuatiwa na Simba iiliyotwaa mara 18 na Mtibwa Sugar ya Morogoro mara mbili.

Yanga imefikia rekodi hiyo baada ya kutwaa ubingwa katika miaka ya 1968, 1969, 1970, 1971, 1972, 1974, 1981, 1983, 1985, 1987, 1989, 1991, 1992,1993, 1996, 1997, 1998, 2002, 2005, 2006 na misimu ya 2007-2008, 2008-2009, 2010-2011, 2012-2013, 2014-15 na 2015-16.

Kwa upande mwingine Malinzi pia amezikumbusha na kuhamamisha klabu zitakazoshiriki Ligi Kuu msimu wa 2016/17 kutoa maoni na mapendekezo, ili kuboresha kanuni za uendeshaji wa ligi hiyo kwa msimu ujao.

Yanga imetwaa ubingwa huo ikiwa na mechi mbili mkononi, dhidi ya Ndanda Jumamosi na Majimaji Mei 22 Uwanja wa Majimaji, Songea.