ALI VELAYATI: JOHN KERRY(USA) HANA HADHI YA KUZUNGUMZIA MAKOMBORA YA IRAN.

ALI VELAYATI: JOHN KERRY(USA) HANA HADHI YA KUZUNGUMZIA MAKOMBORA YA IRAN.

Mshauri wa Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu katika masuala ya kimataifa amesema Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani hana hadhi wala itibari ya kuzungumza chochote kuhusu uwezo wa kujihami wa Iran

Katika mazungumzo na Marina Kaljurand, Waziri wa Mambo ya Nje wa Estonia jijini Tehran hapo jana, Ali Akbar Velayati alisema John Kerry, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani hana nafasi yeyote katika masuala ya kiulinzi ya Iran na haswa uwezo wa makombora wa nch hii.

Kauli ya Velayati imetolewa sambamba na matamshi ya Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Iran ambaye pia jana alisema katu Jamhuri ya Kiislamu haiwezi kufanya aina yoyote ya mazungumzo kuhusu uwezo wake wa makombora. Muhammad Javad Zarif, aliyasema hayo katika kikao cha pamoja na waandishi wa habari na mwenzake Marina Kaljurand wa Estonia mjini Tehran na kuongeza kuwa, suala la makombora ni suala la ulinzi na usalama wa taifa zima la Iran hivyo Jamhuri ya Kiislamu haiwezi kuzungumza na yeyote yule kuhusu cha kufanya au kutofanya.

Marekani katika siku za hivi karibuni imekuwa ikieneza propaganda kuwa kuendelea Iran kujiimarisha kimakombora kunakiuka makubaliano ya nyuklia ya Vienna, yaliyofikiwa kati ya Iran na kundi la 5+1 mwaka jana.

JOKA KUBWA DUNIANI LIMEKUFA.

JOKA KUBWA DUNIANI LIMEKUFA.

Joka kubwa zaidi kuwahi kukamatwa duniani amekufa.

Chatu huyo aliyepatikana katika eneo lililokuwa likijengwa nchini Malaysia karibu na mti mkubwa uliokatwa katika kisiwa cha Penang.

Joka hilo linakisiwa kuwa takriban mita 8 hivi sawa na futi 26 lilipatikana siku ya Alhamisi iliyopita. Kwa bahati mbaya joka hilo lilikufa jumapili lilipokuwa likizaa.

Chatu huyo aliyepatikana katika eneo lililokuwa likijengwa nchini Malaysia
Afisa anayesimamia ujenzi katika kisiwa hicho cha Penang, Herme Herisyam aliiambia BBC.

Kulingana na daftari za kumbukumbu za Guinness, joka anayeshikilia rekodi ya dunia anaurefu wa mita 7.67. Chatu huyo anayeitwa Medusa ana uzani wa kilo 158 na anaishi katika jumba moja mjini Kansas City, Missouri Marekani.

Hata hivyo joka huyo wa Malaysia ambaye alikuwa mkubwa zaidi yake hakuwa amepimwa na kuthibitishwa kuwa mrefu zaidi kabla ya kufa kwake.

Bw Herisyan anasema kuwa alikuwa na uzani wa kilo 250. Hata hivyo katika harakati za kumuokoa kutoka maficho yake inakisiwa kuwa aliumia na hivyo akafa kabla hajafikishwa kwenye hifadhi ya wanyama alikotarajiwa kutuzwa hadi ajifungue.

DAWA YA KUREFUSHA MAISHA IMEGUNDULIWA.

DAWA YA KUREFUSHA MAISHA IMEGUNDULIWA.

Dawa inayotumika kwa matibabu ya kawaida huenda ikategua kitendawili cha kurefusha maisha na kuzuia uzee.
Hii ni kwa mujibu wa utafiti mpya, ambao ulibainisha kwamba viwango vya chini vya dawa aina ya Lithium vilisaidia kurefusha maisha ya nzi waliowekwa kwenye maabara.

Wanasayansi wamesema utafiti huu unatoa matumaini ya kutoa dawa kuwasaidia watu kuishi maisha marefu na yenye afya. Lithium inatumika katika matibabu ya matatizo ya akili, kama mfadhaiko, na kusongwa na mawazo.

Hata hivyo ina madhara makubwa ikiwa itatumika kwa viwango vya juu.
Haijulikani jinsi Lithium inavyotibu matatizo ya akili, lakini alipopewanzi, dawa hiyo ilisaidia kurefusha maisha yao.
Hata hivyo watafiti wamesisitiza lazima dawa hii kutumiwa kwa viwango vya chini zaidi, kwani viwango vya juu vinaweza kuleta maafa.

Dkt Ivana Bjedov mmoja wa watafiti kutoka taasisi ya matibabu ya saratani amesema dawa hii itasaidia afya kwa wazee sawa na kuzuia magonjwa kama vile ugonjwa wa kutetemeka 'Parkinson'.
Kando na matatizo ya akili Lithium imetumika kutibu maumivu makali ya kichwa 'Migraines' na ugonjwa wa jongo unaomfanya mtu kuvimba viungo hasa wakati wa baridi.

RAIS MTUMBUA JIPU ANA KILANGO MALECELA.

Rais Magufuli ametangaza kutengua uteuzi wa Viongozi hao wa Mkoa wa Shinyanga leo tarehe 11 Aprili, 2016 Ikulu Jijini Dar es salaam, mara baada ya kupokea Taarifa ya Mwaka 2014/2015 ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), na kupokea hundi kifani ya shilingi Bilioni 6 kutoka Ofisi ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zilizotokana na kubana matumizi.

Dkt. Magufuli ameeleza kuwa baada ya kupata taarifa kuwa Mkoa wa Shinyanga hauna watumishi hewa, aliamua kutuma timu ya ukaguzi iliyokwenda kufanya uchunguzi ambapo hadi kufikia jana tarehe 10 Aprili, 2016 imebaini kuwepo watumishi hewa 45 huku zoezi likiwa linaendelea katika wilaya mbili za Ushetu na Shinyanga Vijijini.

"Na wale wote wa Shinyanga ambao walisemekana ni zero, hakuna mtumishi hewa, walikuwa tayari wameshalipwa shilingi milioni 339.9, nimejiuliza sana, na nikajiuliza sana na kwa kweli nimejiuliza sana na kwa masikitiko makubwa, kwa nini Mkuu wa Mkoa alisema hakuna mtumishi hewa?" Amesisitiza Rais Magufuli.

Rais Magufuli amesema baada ya kutengua uteuzi wake, Anne Kilango Malecela atapangiwa kazi nyingine.
Pamoja na hatua hiyo, Dkt. Magufuli ametaka wakuu wa mikoa yote wawafichue watumishi hewa wote ili waondolewe mara moja, na ameagiza timu iliyofanya uchunguzi Mkoani Shinyanga itumike kufanya uchunguzi katika mikoa mingine kwa lengo la kukomesha upotevu mkubwa wa fedha za umma.

Katikati ya Mwezi Machi, 2016 Rais Magufuli aliwaagiza wakuu wa mikoa yote nchini kusimamia zoezi la kuwaondoa watumishi hewa wote katika orodha ya malipo ya mshahara, ambapo mpaka tarehe 31 Machi, 2016 Jumla watumishi hewa 5,507 walibanika.
Kati ya shilingi Bilioni 583 ambazo serikali imekuwa ikitumia kila mwezi kwa ajili kulipa mishahara, kati ya shilingi Bilioni 53 na 54 zimekuwa zikipotea kutokana na kulipa mishahara ya watumishi hewa.

Kabla ya kutangaza kutengua uteuzi wa Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga na Katibu Tawala wa Mkoa huo, Rais Magufuli ameipongeza ofisi ya Bunge kwa kubana matumizi na kufanikiwa kuokoa shilingi Bilioni 6, ambazo zitatumika kutengeneza madawati ya wanafunzi wa shule na amezitaka ofisi na taasisi nyingine za serikali kuiga mfano huo.

Ameagiza fedha hizo zipelekwe Idara ya Magereza na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) ili vyombo hivyo vifanye kazi ya kutengeneza madawati yanayotarajiwa kuwa zaidi ya 120,000 ambayo yatasambazwa katika shule ili kukabiliana na tatizo la wanafunzi wanaokaa chini kwa kukosa madawati.

Hundi Kifani ya fedha hizo imekabidhiwa kwa Mheshimiwa Rais na Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Tulia Akson, ambaye amesema Ofisi ya Bunge imetekeleza wito wa serikali wa kubana matumizi ambapo kiasi hicho cha shilingi Bilioni 6 kimepatikana kwa kipindi kifupi cha takribani nusu mwaka.

Katibu wa Bunge Dkt. Thomas Kashilila ametaja maeneo ambayo Bunge limebana matumizi kuwa ni Safari za nje ya nchi, Mafunzo nje ya nchi, Machapisho na ununuzi wa majarida, Shajala, Chakula na Viburudisho, Mtandao, Malazi hotelini, Matibabu ya wabunge na familia zao nje ya nchi, Umeme, Maji, Simu na Uendeshaji wa Mitambo.

MAHARAMIA WATEKA MELI YA UTURUKI KATIKA PWANI YA NIGERIA.

MAHARAMIA WATEKA MELI YA UTURUKI KATIKA PWANI YA NIGERIA.

Maharamia katika pwani ya Nigeria wameshambulia meli ya mizigo ya Uturuki na kuwateka nyara wafanyikazi sita wa meli hiyo, katika eneo hilo ambalo limeshuhudia visa vingi vya uharamia miaka ya hivi karibuni.

Shirika la habari la Deniz lilisema kuwa wale waliotekwa nyara walikuwa ni pamoja na mhandisi ya mitambo, fundi wa umeme pamoja na muelekezi.

Meli hiyo inamiikiwa na kampuni ya Kaptanogul, ambayo ililiambia shirika hilo la habari kuwa wale waliotekwa nyara pamoja na wale waliosalia melini wote wako katika hali nzuri ya afya.

Haijulikani ni wafanyikazi wangapi walikuwa ndani ya meli hiyo, ambayo ilikuwa ilikuwa ikisafirisha kemikali wakati iliposhambuliwa, kwa mujibu wa shirika la habari la AFP.

WAZIRI MKUU WA PAKISTANI ATAKIWA KUJIUZULU.

WAZIRI MKUU WA PAKISTANI ATAKIWA KUJIUZULU.

Mpinzani mkuu wa kisiasa nchini Pakistan, Imran Khan, amemtaka Waziri Mkuu wa nchi hyo Nawaz Sharif kujiuzulu.

Shauri hilo limetolewa baada ya nyaraka zilizotolewa kwa siri na kituo cha sheria cha Panama kufichua kwamba watoto wake mwenyewe wanamiliki kampuni kadhaa katika nchi ya nje.

Ufichuaji huo umezua mjadala mkubwa nchini Pakistan katika duru za kisiasa na vyombo vya habari ukimkosoa waziri mkuu Sharif kwa kudaiwa kuficha mali za familia yake kwa siri.

Waziri mkuu huyo amepinga madai yoyote ya uwajibikaji wake ama wa watoto wake wa kiume usio sahihi.

Wiki iliyopita alitangaza kuanzishwa kwa tume ya sheria itakayoongozwa na jaji mstaafu kuchunguza kashfa hiyo.

Lakini mpinzani wake mkuu Imran Khan, katika hotuba kupitia televishani amepinga kuundwa tume hiyo akisema ni jaribio la kuficha ulaji rushwa umaofanywa na familia ya Sharif.

WITNES AFUNGUKA KUHUSU PICHA, ASEMA HAWEZI KUMRIDHISHA KILA MTU.

WITNES AFUNGUKA KUHUSU PICHA, ASEMA HAWEZI KUMRIDHISHA KILA MTU.

Witness ameyasema hayo katika kipindi cha Planet Bongo kinachorushwa na East Africa Radio, na kusema kuwa alipost picha hiyo akiwa na lengo la kuwaonyesha watu ni jinsi gani amepungua na kuwaelimisha nini cha kufanya, lakini watu wameichukulia tofauti.

Pia msanii huyo amesema hawezi kumzuia mtu kuwa na mtazamo tofauti kwa kupost picha hiyo, kwani binadamu wanatofautiana kimawazo.

“Ni kwamba sisi binadamu tuko tofauti hauwezi ukamridhisha kila mtu, mimi nimeweka kwa lengo la kuelimisha kuhusiana na masuala ya kupungua, mwengine anaona kwa lengo lake yeye mwenyewe tofauti, kwa hiyo malengo yanatofautiana, unaweza ukafanya kitu ukaona hiki kitu kizuri, mwengine akaona kitu kibaya, so now nimeweka hiyo picha kila mtu anasema kivyake, I dont real understand”, alisema Witness.

Pia Witness amewataka watu watambue kuwa pamoja na wao kuwa wasanii lakini wana maisha yao mengine, na kuwataka wamuache aishi maisha yake.

“Unatakiwa ufike wakati ambao watu wajue kabisa kwamba sometimes nina vitu ambavyo nnaweza nikaamua kuvifanya, so can they just leave me alone.”, alisema Witness.

OBAMA AJUTIA ALICHOKIFANYA LIBYA YEYE NA WAITIFAKI WAKE.

OBAMA AJUTIA ALICHOKIFANYA LIBYA YEYE NA WAITIFAKI WAKE.

Rais wa Marekani Barack Obama amekiri kwa mara ya kwanza kwamba serikali yake ilifeli katika kutatua mzozo wa Libya.
Amesema hilo huenda ndilo “kosa kubwa” zaidi alilolitenda wakati wa utawala wake.

Bw Obama amesema Marekani haikua na mpango mahususi wa jinsi taifa hilo litakavyotawaliwa baada ya kuondolewa madarakani kwa Kanali Muammar Gaddafi.

Alisema haya katika mahojiano na runinga ya Fox News kuangazia mafanikio na mapungufu ya utawala wake.

Eneo la Sirte, alikozaliwa Gaddafi, lilishambuliwa sana na majeshi ya muungano. Hata hivyo ametetea hatua ya kuingilia kijeshi nchini Libya. Marekani na Muungano wa NATO zilitekeleza mashambulio ya anga kuwalinda raia baada ya kuzuka maasi dhidi ya Muammar Gaddafi mwaka 2011.

Lakini baada ya mauaji ya kiongozi huyo, Libya ilitumbukia katika vita vya wenyewe kwa wenyewe kati ya makundi ya waasi huku makundi mawili yakiunda serikali na mabunge tofauti.

Katika hatua za kurejesha utulivu serikali ya muungano wa kitaifa inayoungwa mkono na Umoja wa Mataifa imewasili katika mji mkuu Tripoli ili kuanza mipango ya kuongoza nchi ya kurejesha hali ya kawaida.

Uchaguzi mkuu nchini Marekani utafanyika Novemba na Rais Obama atakabidhi madaraka kwa mrithi wake Januari mwakani baada ya kuongoza kwa mihula miwili.

MANYARA WAPEWA MWEZI MMOJA KUKUSANYA DAMU SALAMA.

MANYARA WAPEWA MWEZI MMOJA KUKUSANYA DAMU SALAMA.

Dkt. Kigwangala amesema hayo baada ya kutembelea hospitali ya rufaa ya mkoa wa Manyara, iliyopo mjini Babati na kushuhudia hospitali hiyo ikiwa haina damu ya kutosha kwenye benki yake.
Naibu Waziri huyo amemtaka Mganga Mkuu wa Mkoa huo Dkt. Ally Uledi, kuanisha mipango ya upatikani wa damu salama katika kipindi cha siku 30,baada ya kushuhudia benki ya damu ikiwa na unit 3 badala ya 150 zinazohitajika.

Aidha, Dkt. Kigwangala ameuagiza uongozi wa hospitali hiyo ya rufaa ya mkoa kuwa na chumba maalumu cha kuwahudumia wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalum ambapo amesema wajenge walau vyumba viwili kwa ajili ya shughuli hiyo.

Dkt. Kigwangala amesema kuwa kutokana na hospitali kuhudimia idadi kubwa ya watu haiwezi kufanya kazi ikiwa haina damu ya kutosha vitanda vya kutosha na hata chumba maalum cha wagonja wanaohitaji uangilizi maalum hivyo mkoa huo hauna budi kufanya juu chini kuweza kutatua changamoto hiyo.