ALI VELAYATI: JOHN KERRY(USA) HANA HADHI YA KUZUNGUMZIA MAKOMBORA YA IRAN.

ALI VELAYATI: JOHN KERRY(USA) HANA HADHI YA KUZUNGUMZIA MAKOMBORA YA IRAN.

Mshauri wa Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu katika masuala ya kimataifa amesema Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani hana hadhi wala itibari ya kuzungumza chochote kuhusu uwezo wa kujihami wa Iran

Katika mazungumzo na Marina Kaljurand, Waziri wa Mambo ya Nje wa Estonia jijini Tehran hapo jana, Ali Akbar Velayati alisema John Kerry, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani hana nafasi yeyote katika masuala ya kiulinzi ya Iran na haswa uwezo wa makombora wa nch hii.

Kauli ya Velayati imetolewa sambamba na matamshi ya Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Iran ambaye pia jana alisema katu Jamhuri ya Kiislamu haiwezi kufanya aina yoyote ya mazungumzo kuhusu uwezo wake wa makombora. Muhammad Javad Zarif, aliyasema hayo katika kikao cha pamoja na waandishi wa habari na mwenzake Marina Kaljurand wa Estonia mjini Tehran na kuongeza kuwa, suala la makombora ni suala la ulinzi na usalama wa taifa zima la Iran hivyo Jamhuri ya Kiislamu haiwezi kuzungumza na yeyote yule kuhusu cha kufanya au kutofanya.

Marekani katika siku za hivi karibuni imekuwa ikieneza propaganda kuwa kuendelea Iran kujiimarisha kimakombora kunakiuka makubaliano ya nyuklia ya Vienna, yaliyofikiwa kati ya Iran na kundi la 5+1 mwaka jana.