TAARIFA ZA SASA KUHUSU NDEGE YA MISRI ILOPOTEA.


Wanajeshi wa Misri na maafisa wa Uigiriki wanatafuta ndege ya shirika la EgyptAir iliotoweka ikitoka mjini Paris Ufaransa kuelekea Cairo Misri ikiwa na abiria 66.

Ugiriki imetuma ndege mbili na pia itatuma meli moja eneo hilo ili kusaidia utafutaji kwenye bahari ya Mediterranean ambako inaaminika huenda ndege hiyo ilianguka.

Nchini Ufaransa mamlaka zinaandaa mkutano wa dharura kujadili kutoweka kwa ndege hiyo.

Waliokuwemo kwenye ndege hiyo aina ya Airbus A320, ni pamoja na Wamisri 30 Wafaransa 15, Mwingereza 1, Mbelgiji 1,Wairaqi 2, Mkuwait 1, Msaudi 1, Msudan 1,Raia wa Chad 1,Mreno 1,Raia wa Algeria 1, na raia wa Canada 1.

Ilikuwa ikisafiri kutoka Ufaransa kwenda Misri na kutoweka kwenye mtambo wa rada kilomita 280 hivi kabla ya kufika pwani ya Misri.

Rais wa Ufaransa Francois Hollande na mwenzake wa Misri Abdul Fattah al-Sisi wamewasiliana na kuahidi kushirikiana katika uchunguzi, hayo ni kwa mujibu wa shirika la Reuters .

NDEGE YA MISRI YAPOTEA KWENYE RADA, HAUJULIKANI ILIPO

Ndege ya abiria ya shirika la EgyptAir iliyokuwa imebea abiria 56 na wahudumu 10 wakiwemo marubani imetoweka kwenye rada, ikitokea mji mkuu wa Ufaransa Paris kuelekea Cairo, mji mkuu wa Misri.

Gazeti la serikali la Ahram limeripoti kuwa, ndege hiyo yenye nambari ya usajili A320, ilikuwa inaruka umbali wa mita 11,300 kabla ya kutoweka kwenye rada, mashariki mwa bahari ya Mediterranean, maili 10 kabla ya kuingia kwenye anga ya Misri. Maafisa wa Idara ya Safari za Anga nchini Misri wamesema yumkini ndege hiyo imeanguka katika bahari hiyo.

Kwa mujibu wa Wizara ya Uchukuzi ya Misri, abiria waliokuwa kwenye ndege hiyo ni pamoja na Wamisri 30, raia 15 wa Ufaransa na Muingereza mmoja.

Itakumbukuwa kuwa, ndege nyingine ya abiria ya shirika la Metrojet la Russia nambari A321, ilianguka katika Peninsula ya Sinai nchini Misri Oktoba 31 mwaka jana, na kuua watu wote 224 waliokuwemo kwenye ndege hiyo.

Aidha ndege nyingine ya abiria ya shirika la EgyptAir iliyokuwa na abiria 55 na wahudumu 7 ambayo ilikuwa inatoka Alexandria kwenda jijini Cairo, ilitekwa nyara na raia wa Misri ambaye aliaminika kuwa na akili taahira kwa jina Seifuddin Mustafa ambaye alidai kuwa alifanya hivyo ili kuishinikiza serikali ya Cairo iwaachie huru wafungwa wa kisiasa kabla ya kubadili kauli yake na kusema kuwa alitaka aletewe mtalaka wake raia wa Cyprus waonane katika uwanja wa ndege wa kisiwa hicho.  

Mama mzazi wa binti aliyebakwa Morogoro alitumiwa video na kuipeleka polisi

Mama mzazi wa binti mmoja mkazi wa Dakawa wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro hivi karibuni alipokea ujumbe wa picha ya video katika simu yake ya mkononi na haraka aliifungua akiwa na shauku ya kuitazama.

Lahaula! Shauku yake ya kuitazama video hiyo aliyodhani ni sawa na nyingine za matukio ambazo amekuwa akiziona zikisambazwa mitandaoni, iligeuka huzuni na fedheha kubwa alipoona ikimwonyesha bintiye akidhalilishwa na wanaume huku akilalamika asirekodiwe bila mafanikio.

Mama huyo alijizoazoa haraka na simu yake akatimua mbio hadi Polisi kuripoti tukio hilo lililolenga kumdhalilisha binti yake na kuifedhehesha familia nzima. Hicho ndiyo kiini cha vijana 11 wa Dakawa kukamatwa ili waisaidie Polisi kuhusu walioshiriki tukio hilo na walioisambaza video hiyo kwa mama huyo na kwenye mitandao ya kijamii hasa WhatsApp.

Katika video hiyo, wakati mwanamme mmoja akimdhalilisha huyo binti, mwingine alikuwa akirekodi na baada ya kukamilisha tendo hilo lisilo na utu tena bila huruma waliwatumia watu wengine katika eneo la Dakawa.

Mkuu wa Wilaya ya Mvomero, Betty Mkwasa aliliambia gazeti hili jana kuwa miongoni mwa watu wa kwanza kuona video ile alikuwa mama wa msichana. “Alikimbia polisi kwenda kutoa taarifa,”alisema Betty.

Baada ya kufika Polisi, Betty alisema polisi walimwambia mama huyo hawawezi kuandika maelezo hadi mhusika ambaye ni binti yake afike kituoni. Walisema hivyo kwa sababu ni mtu mzima hivyo anatakiwa kutoa maelezo mwenyewe. Saa chache baada ya kuandikisha maelezo yake, polisi waliwakamata vijana wawili kwa tuhuma za kuhusika na unyama huo. Betty alisema watuhumiwa hao walikamatwa juzi na leo watafikishwa mahakamani.

Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Morogoro, Ulrich Matei alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba suala hilo linaendelea kufanyiwa kazi na kwamba hadi jana watuhumiwa 11 walikamatwa kuhusiana na tukio hilo.

Kamanda Matei alisema tisa kati yao wanaoshikiliwa ni kwa kosa la kusambaza picha za utupu huku vijana wawili ambao ni Zuberi Thabiti (30) na Iddy Adamu (32) ni kwa kosa la kufanya mapenzi na msichana huyo kwa nguvu huku wakirekodi.

Ilivyokuwa

Akisimulia tukio hilo, Kamanda Matei alisema kuwa watuhumiwa hao walifanya kitendo hicho Aprili 28 mwaka huu majira ya saa 1.00 usiku katika nyumba ya kulala wageni yenye jina la ‘Titii’ iliyopo Dakawa.

Kamanda Matei alisema kuwa binti huyo aliitwa kwenye nyumba hiyo ya wageni na Thabiti ambaye ni mkazi wa Mbarali wilaya ya Mbeya ambaye alikuwa na uhusiano naye kimapenzi. Baada ya kuingia chumbani alimkuta pia Adamu mkazi wa Makambako, Njombe ambao walimlazimisha kufanya mapenzi huku mmoja akimrekodi picha za video na baadaye kuzisambaza kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii.

Wanaoshikiliwa kwa kosa la kusambaza picha za utupu ni Rajabu Salehe (26), Said Athman (26), Musi Ngai (36), Said Muhammed (24), John Peter (24), Hassan Ramadhan (27), Ramadhan Ally (26), Lulu Peter (38) na Magreth Njonjone (30).

Wote ni wakazi wa Dakawa, Morogoro na wamevunja Sheria ya Makosa ya Mitandao, kifungu namba 14, kifungu kidogo (1) (a)

Kamanda Matei alisema wakati wa tukio hilo watuhumiwa hao walimtisha binti huyo kwa kisu ili asipige kelele wakati akidhalilishwa na walimtaka asitoe siri hiyo vinginevyo watamuua.

Kamanda alisema wawili hao ni marafiki wa msichana huyo na kwamba Thabiti ambaye ni mpenzi wa sasa wa msichana huyo alipanga na Adamu ambaye ni mpenzi wake wa zamani kumkomesha.

Alisema Thabiti alimwambia mpenzi wake wakutane hotelini. Msichana alipofika aliwakuta chumbani huku Adamu akiwa ameshika kisu na kamera. “Wakamlazimisha afanye vile na kumtishia kumuua kama angekataa,”alisema Matei.

Hata hivyo, Betty alisimulia kisa hicho na kusema watuhumiwa hao walifanya unyama huo kwa sababu ya usaliti wa mapenzi. Alisema msichana alidaiwa kujihusisha kimapenzi na dereva wa mpenzi wake.

Kwa mujibu wa Betty, baada ya mpenzi wake kugundua alipanga njama ili kuwakomoa wote wawili. Alisema mpenzi wake alimwambia wakutane hotelini na alipofika alimkuta Zuberi pamoja na dereva wa mchumba wake hotelini.

“Akawambia wafanye kile kitendo huku akirekodi video,”alisema Betty. “Nia yake ilikuwa kuwakomoa…kwa nini atembee na dereva wake,”alisema Betty na kwamba baada ya hapo picha hizo zilianza kusambaa.

Akizungumzia tukio hilo, Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk Hellen Kijo-Bisimba alisema hali hiyo inaonyesha jinsi maadili yanavyozidi kuporomoka katika jamii.

“Hilo siyo kosa la kisheria peke yake ni udhalilishaji mkubwa,”alisema.

Dk Hellen alisema licha ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu kukemea suala hilo ni vyema jamii ikazingatia suala la maadili.

Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA), Edda Sanga alisema vyama vya kutetea haki za wanawake vinafanya mkutano wa pamoja kujadili suala hilo.

“Leo (jana) tumekutana ili tujadili na kuja na tamko la pamoja,”alisema Sanga na kuongeza kwamba jambo hilo halivumiliki kwa sababu vitendo kama hivyo vinaendelea kujitokeza mara kwa mara.
  • Imenukuliwa kutoka gazeti MWANANCHI

RWANDA: HATUJA WATIMUA WAKIMBIZI.


Serikali ya Rwanda imekanusha madai kwamba, imewafukuza kutoka nchini humo wakimbizi kutoka Burundi.

Taarifa ya serikali ya Rwanda imesisitiza kwamba, haijawafukuza wakimbizi kutoka Burundi na kwamba wanaofukuzwa kutoka nchini humo ni raia wa Burundi wasio na vibali vya kuishi nchini humo.

Gavana wa jimbo la kusini mwa Rwanda ambako zaidi ya raia 1000 kutoka Burundi wamekwishatimuliwa ameziambia duru za habari kwamba, wanaofukuzwa walitakiwa kupata vibali vya kuendelea kuishi nchini humo na kisha warejee ikiwa watapenda.

Hivi karibuni Gavana wa mji wa Kirundo wa Burundi ambao uko katika mpaka wa nchi hiyo na Rwanda alisema kuwa, Rwanda imewatimia wakimbizi 1,300 wa Burundi ambao walitakiwa kurejea katika kambi za wakimbizi au kuondoka nchini humo. Melchior Nankwahomba alisema wale waliokataa kwenda katika kambi za wakimbizi walikuwa wakiondolewa kwa nguvu na maafisa wa Rwanda.

Makumi kwa maelfu ya Warundi walikimbilia Rwanda tangu ghasia zilipoanza nchini mwao mwaka mmoja uliopita, kufuatia uamuzi wa Rais Pierre Nkurunziza wa kuwania Urais kwa muhula wa tatu mfululizo hatua ambayo ililalamikiwa na wapinzani waliosema ilikiuka katiba na makubaliano ya amani ya Arusha Tanzania.

Burundi imekuwa ikiituhumu Rwanda kwamba, inaingilia masuala yake ya ndani, madai ambayo yanakanushwa na serikali ya Kigali.

KENYA YAPATA PIGO LINGINE, BAADA YA BOMBA LA MAFUTA, SASA RELI.


Rwanda imetangaza kuwa itajenga njia ya reli ya kisasa aina ya SGR kupitia Tanzania badala ya Kenya ikisema kuwa njia ya Tanzania itahitaji bajeti ya chini ikilinganishwa na Kenya.

Akihutubia waandishi wa habari hapo jana, waziri wa fedha wa Rwanda Claver Gatete, aliongeza kuwa itachukua muda kidogo kujenga reli hiyo kupitia Tanzania badala ya Kenya.

Utafiti uliofanywa na nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki umeonyesha kuwa njia ya Tanzania itagharimu Rwanda kati ya dola milioni 800-900 huku njia ya Kenya ikigharimu dola bilioni moja. Njia hiyo ya reli itakayotoka Dar es Salaam-Isaka-Kigali/Keza-Musongati (DIKKM) itakamilishwa mwaka wa 2018 na inatarajiwa kugharimu nchi husika jumla ya dola bilioni 5.2.

KISO CHAKO HUKISHIKI

Ufanye uende mbio, kaskazi mashariki,
Ubebe na kuku kwio, kwa ndumba unihiliki,
Yote yawa kifagio, kwa uwezo wa Maliki,
Jalali sio babio, elewa sihadhiriki.
Kiso chako hukishiki, hata kwa lake shikio.

Mja kalisha kalio, hazina pato shiriki,
Fanya uweke fungio, huta zuia riziki
Waja angua kilio, useme na hizo chuki,
Mola wangu kimbilio, wallahi sifedheheki,
Kiso chako hukishiki, hata kwa lake shikio.

Nimegundua mwenzio, tabasamu lako feki,
Watia kinukajio, kwa chips na mishikaki,
Umepaka kipambio, sumu nipate fariki,
Rabi kahuluku "sio" ndio mana sianguki
Kiso chako hukishiki, hata kwa lake shikio.

Ulo nalo kusudio, fahamu halisomeki,
Uweke na kikingio, kiso chako hukishiki,
Ingia kwa kitubio, umrudie Razaki,
Jalali kaumba "ndio" kwahivyo sitetereki.
Kiso chako hukishiki, hata kwa lake shikio.

Wanisema kwa wenzio, vile isivyo stahiki,
Mithili ya kisusio, mdomoni sikutoki,
Neno mwenziwe sikio, halichomi si mkuki,
Mungu tanipa tulio, hakika sibabaiki.
Kiso chako hukishiki, hata kwa lake shikio.

Umeshika mchinjio, na bado haushutuki,
Chakughuri kilalio, kiumbe hauzinduki,
Punguza matamanio, dunia haibebeki,
Rabi nipe kifutio, nifute zako falaki
Kiso chako hukishiki, hata kwa lake shikio.

Alokupa mtwangio, na kinu simdhihaki,
Kuna siku ya chungio, kiumbe huiepuki,
Hivyo situpe dekio, kesho haitabiriki,
Hapa pana zingatio, wajibu nduguye haki,
Kiso chako hukishiki, hata kwa lake shikio.

Dotto Rangimoto Chamchua(Njano5)
0622845394 Morogoro

ISRAELI YAFANYA MASHAMBULIZI UKANDA WA GAZA.


Wanajeshi wa utawala wa Kizayuni kwa kushirikiana walowezi wa Kizayuni wenye chuki za kidini na kitaifa, wamefanya mashambulizi katika maeneo tofauti ya Ukanda wa Ghaza na Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan dhidi ya Wapalestina.

Shirika la habari la WAFA limeripoti habari hiyo na kuongeza kuwa, wanajeshi wa utawala wa Kizayuni walioko katika mpaka unaotenganisha Ukanda wa Ghaza na ardhi nyingine za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu na Wazayuni, leo asubuhi wamevunja makubaliano ya kusimamisha vita kwa kuwashambulia wakulima wa Kipalestina, mashariki mwa Khan Yunus na kusini mwa eneo hilo, na kuwazuia kuingia kwenye mashamba yao.

Aidha leo asubuhi, wanajeshi wa utawala wa Kizayuni wamewashambulia kwa risasi wakulima wa Kipalestina mashariki mwa eneo la al Shujaiyya, katika Ukanda wa Ghaza.

Hadi sasa hakuna habari zozote zilizotangazwa kuhusu hasara iliyosababishwa na mashambulizi hayo ambayo ni uvunjaji wa wazi wa makubaliano ya kusimamisha vita.

Wakati huo huo walowezi wa Kizayuni leo wamezivamia nyumba za Wapalestina katika mji wa al Khalil wa kusini mwa Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan.

Licha ya walowezi hao wa Kizayuni kusaidiwa na wanajeshi wa utawala wa Kizayuni katika uvamizi huo, lakini Wapalestina wamesimama kidete kukabiliana nao, jambo ambalo limezusha mapigano baina ya pande hizo mbili.

WANANCHI WA YEMEN WASISITIZA KUPAMBANA NA MAREKANI.


Imam wa Sala ya Ijumaa iliyosaliwa jana huko San'a, mji mkuu wa Yemen amesema kuwa, wananchi wa nchi hiyo wataendelea kusimama kidete kupambana na wavamizi wa nchi yao.

Televisheni ya al Maseera ya Yemen imetangaza habari hiyo leo Jumamosi na kumnukuu Sheikh Abdul Majid al Houthi akiwaonya wanajeshi wa Marekani walioivamia ardhi ya Yemen kwamba wananchi wa nchi hiyo kamwe hawataruhusu hata shibri moja ya ardhi ya nchi yao ikaliwe na wavamizi.

Imam wa Sala ya Ijumaa ya San'a ameongeza kuwa, Marekani ina lengo la kuigawa vipande vipande nchi ya Yemen, lakini wananchi wa nchi hiyo wataendelea kuwa kitu kimoja mbele ya njema za Marekani.

Siku chache zilizopita, duru za habari za Yemen zilitangaza habari ya kuingia helikopta 15 aina ya Apache na helikopta 5 aina ya Black Hawk za jeshi la Marekani katika kambi ya jeshi la anga ya al Anad, kusini mwa Yemen.

Siku ya Jumamosi ya wiki iliyopita pia, wanajeshi 200 wa Marekani waliingia katika Ghuba ya Aden sambamba na kuwasili manowari ya kivita ya Marekani katika ghuba hiyo.

Imam wa Sala ya Ijumaa ya mjini San'a amesema, uvamizi huo wa Wamarekani nchini Yemen ulitabiriwa tangu zamani na wananchi wa nchi hiyo na ndio maana kwa zaidi ya mwaka mmoja sasa waendelea kukabiliana na wavamizi wa nchi yao.

BODABODA WANNE WAFA KWENYE MAANDAMANO HUKO CONGO DRC


Watu wanne wameripotiwa kuuawa katika maandamano ya waendesha pikipiki dhidi ya askari wa barabarani, huko mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Maandamano hayo yaliyoitishwa kwa ajili ya kulalamikia miamala mibaya ya polisi wa barabarani, yalifanyika katika barabara kuu ya eneo la Mambasa katika mkoa wa Orientale, kaskazini mashariki mwa nchi hiyo. Waandamanaji hao wanawatuhumu polisi kwamba wanachukua kiasi kikubwa cha fedha sawa na faranka 2000 kwa pikipiki moja ili kuruhusiwa kupita kwenye moja ya vizuizi kwenye eneo hilo, kiwango ambacho wanadai ni kikubwa kulingana na kipato chao.

Aidha madereva hao wa pikipiki (maarufu kama bodaboda) wametaka pia kuachiliwa huru pikipiki kadhaa ambazo zinashikiliwa na jeshi hilo la polisi wa barabarani katika eneo hilo. Katika kumaliza maandamano hayo, polisi hao wa barabarani walifyatua risasi kuwalenga waandamanji. Kiongozi wa eneo hilo la Mambasa, Alfred Bongwalanga amethibitisha kutokea machafuko hayo na watu wanne kuuawa.

Bongwalanga amesema kuwa, zaidi ya madereva 500 wa pikipiki walishiriki katika maandamano hayo. Baadhi ya vyombo vya habari vimesema kwamba, kulikuwa kumeshuhudiwa moto kwenye kituo kimoja cha polisi, kabla ya polisi kudhibiti eneo la PK51 katika mji huo wa Mambasa.